JUMLA ya Sh 16.2 bilioni zimetolewa na Serikali kwa ajili ya kulipa fidia kwa wananchi ambao watapisha ujenzi wa barabara mbalimbali nchini. Anaripoti Danson Kaijage, Simiyu …(endelea).
Hayo yameelezwa Waziri wa Ujenzi, Innocent Bashungwa katika ziara ya kikazi mkoani Simiyu ya ukaguzi wa miradi ya barabara na kuzungumza na wananchi pamoja na wakandarasi.
Bashungwa alikagua utelelezaji wa ujenzi wa barabara ya mchepuo (Maswa Bypass) yenye urefu wa kilometa 11.3 kwa kiwango cha lami ambao ujenzi umefikia asilimia 99.
Aidha, Bashungwa ameeleza kuwa lengo la Serikali la kuijenga barabara ya mchepuo ya Maswa (Maswa Bypass) ni kupunguza msongamano wa magari yanayopita katikati ya mji wa Maswa.
Amesema Serikali tayari imetenga fedha kwa ajili ya kuanza upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa bararara ya Bariadi-Salama-Mhayo-Magu (km 76), Bariadi-Itilima-Mwandoya-Moroco (km 104), Nyashimo-Ngasamo-Ndutwa (km 48) ili kupata gharama za ujenzi wake kwa kiwango cha lami.
Akitoa taarifa ya mradi, Meneja wa Wakala wa Barabara (TANROADS), mkoa wa Simiyu, Mhandisi John Mkumbo ameeleza kuwa mkataba wa ujenzi wa barabara hiyo ulisainiwa kati ya TANROADS na Mkandarasi kampuni ya CHICO tarehe 1 Juni, 2021 kwa gharam ya Sh 13.4 bilioni.
Ameongeza kuwa mkandarasi anaendelea kumalizia kazi ndogo ndogo za kuweka alama za barabarani, kuchora mistari ya usalama barabarani pamoja na kujenga miundombinu saidizi ya barabara.
Leave a comment