WAKULIMA katika mabonde ya Bugwema na Suguti, katika Wilaya ya Musoma mkoani Mara, wameiomba Serikali kuharakisha ujenzi wa miundombinu ya umwagiliaji ili iwasaidie kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabia ya nchi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mara … (endelea).
Ombi hilo limetolewa mwishoni mwa juma lililopita, wakati timu ya watalaamu kutoka serikalini ilipokwenda kwenye mabonde hayo kwa ajili ya kufanya upembuzi yakinifu ili ujenzi uanze.
Thomas Mauna, alisema “tunamshukuru sana Rais Samia kwa kukubali kujenga miundombinu kwenye mabwawa haya, badala ya kutgemea mvua za Mungu. Kila siku mazao yanasubiri mvua na hali ya hewa inazidi kuleta ukakasi. Tunaomba Serikali ituharakishie huu mradi uishe mapema.”
Naye William Kipchoge alisema ujenzi huo utakapokamilika utawasaidia kulima mazao katika misimu yote, kitendo kitakacholeta usalama wa chakula nchini.
“Kwa kweli nimefarijika sana moyoni kwamba Serikali inatambua umuhimu wa kilimo cha umwagiliaji na kwa sababu hiyo tutafukuza njaa katika eneo hili na bonde litaweza saidia maeneo mengine,” alisema mkulima mwingine, Rafael Masige.
Mbunge wa Musoma Vijijini, Prof. Sospeter Muhongo, alisema mradi huo ukikamilika utasaidia wenyeji wa maeneo hayo pamoja na wageni.
“Nimeomba wizarani kwamba hapa kitakuwa kilimo cha umwagiliaji kwa wakulima wadogo wanaoishi humo na wenyewe wa hapo na hakuna atakayehamishwa. Hayo ndiyo makubaliano yangu na wizara pamoja na wakulima wakubwa watakaoletwa,” alisema Prof. Muhongo.
Leave a comment