RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, kesho Jumatatu tarehe 2 Agosti, 2021, anafanya ziara ya rasmi ya Kiserikali ya siku mbili nchini Rwanda kwa mwaliko wa Rais wa nchi hiyo, Paul Kagame. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa ya Jaffar Haniu, Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu aliyoitoa leo Jumapili, tarehe 1 Agosti 2021, imesema, Rais Samia pamoja na mambo mengine atafanya mazungumzo rasmi na mwenyeji wake, Rais Kagame.
Pia, atashuhudia utiaji saini wa hati za makubaliano na kuzungumza na vyombo vya habari.
Haniu amesema, ziara hiyo ya siku mbili inalenga kuimarisha zaidi uhusiano na ushirikiano baina ya Rwanda na Tanzania.
Hii ni ziara ya nne ya Rais Samia kuifanya tangu alipoingia madarakani tarehe 19 Machi 2021, akichukua nafasi ya aliyekuwa Rais, Hayati John Pombe Magufuli.
Hayati Magufuli, alifariki dunia tarehe 17 Machi 2021, katika Hospitali ya Mzena, Dar es Salaam kisha mwili wake, kuzikwa nyumbani kwao, Chato mkoani Geita.
Nchi zingine ambazo Rais Samia amezitembelea ni Kenya, Uganda na Burundi. Nchi zote hizo ni miongoni mwa zinazounga Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC).
Mbali na ziara hizo, tarehe 23 Juni 2021, Rais Samia alikuwa nchini Msumbiji, kushiriki mkutano wa dharura wa wakuu wa nchi na Serikali wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC).
Leave a comment