USAFIRI wa baharini umesimamishwa kwa muda ili kukwepa athari za kimbunga Hidaya kinachozidi kusogea katika Pwani ya Tanzania. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Jana tarehe 3 Mei 2024, Wakala wa Ufundi na Umeme Tanzania (TEMESA), umesimamisha huduma zinazotolewa na vivuko katika baadhi ya maeneo ya mikoa ya Mtwara, Lindi, Tanga, Dar es Salaam na Pwani ikijumuisha visiwa vya Mafia.
Usitishwaji huo wa usafiri wa baharini umekuja baada ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), kutangaza uwepo wa Kimbunga Hidaya karibu na Pwani ya nchi ambacho kinatarajiwa kuathiri mifumo ya hali ya hewa ikiwa pamoja na kusababisha vipindi vya mvua kubwa, upepo mkali utakaoambatana na mawimbi makubwa ya bahari.
“Kutokana na kuwepo kwa tahadhari hiyo ya TMA, TEMESA unawajulisha watumiaji wa vivuko katika baadhi ya maeneo ya Pwani kwamba, kutakuwa na kusimama kwa utoaji wa huduma ya vivuko katika maeneo hayo ili kujilinda na kuepukana na athari zozote ambazo zinaweza kujitokeza kutokana na kimbunga Hidaya na kusababisha athari kwa watumiaji wa vivuko,” imesema taarifa ya TEMESA.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, TEMESA inaendelea kufuatilia taarifa za hali ya hewa zinazoendelea kutolewa na TMA ili kuhakikisha abiria wote wanaotumia huduma hizo wanakuwa salama wakati wote.
Tangu TMA itabiri ujio wa kimbunga hicho ambacho kinatarajiwa kuisha tarehe 6 Mei 2024, tayari dalili zake zimeanza kuonekana kwa uwepo wa upepo mkali katika baadhi ya maeneo ya Pwani, ikiwemo ya mkoa wa Dar es Salaam na visiwa vya Mafia.
Kabla ya TMA kutoa utabiri huo, visiwa vya Mafia vilikabiliwa na changamoto ya upepo mkali hususan baharini na kupelekea shughuli za uvuvi kusimama.
Leave a comment