JIMBO la Musoma Vijjiini mkoani Mara, limeomba Serikali ianzishe shule za kidato cha tano na sita, huku likisema kuna baadhi ya shule zilizojengwa jimboni humo ziko tayari kupokea wanafunzi wa ngazi hiyo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mara… (endelea).
Ombi hilo limetolewa hivi karibuni na Ofisi ya Mbunge Jimbo la Musoma Vijijini, Prof. Sospeter Muhongo, wakati ikitoa taarifa ya maendeleo ya ujenzi wa shule za sekondari unaofanywa na wananchi kwa kushirikiana na Serikali.
“Musoma Vijijini inaomba ipewe High Schools za masomo ya sayansi, sekondari sita zilizotajwa hapo juu ziko tayari kuanza kupokea Wanafunzi wa kidato cha tano na sita mwakani, Julai 2024,” imesema taarifa hiyo.
Katika hatua nyingine, ofisi hiyo imeomba Halmashauri ya Wilaya ya Musoma, kuwaunga mkono wananchi katika ujenzi wa shule hizo kwa kutumia mapato ya ndani.
“Halmashauri yetu (Musoma DC) inaendelea kushawishiwa na kuombwa nayo ianze kuchangia, kwa kutumia mapato yake ya ndani, ujenzi wa Maabara na Maktaba kwenye shule zetu,” imesema taarifa hiyo.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, wananchi kwa kushirikiana na Serikali pamoja na mbunge wao, wamefanikiwa kukamilisha ujenzi wa maabara za sayansi katika sekondari tano za kata, ikiwemo Sekondari za Mugango, Bugwema na Kiriba, huku Sekondari ya Makojo ikitarajiwa kukamilisha ujenzi huo mwishoni mwa Julai 2023.
Pia, ujenzi wa maabara za sayansi katika sekondari nyingine 19 unaendelea, ambao unatarajiwa kukamilisha kabla ya Julai 2023.
Hali kadhalika, wananchi wa jimbo hilo kwa kushirikiana na Serikali wanajenga shule nne mpya za sekondari, zikiwa na majengo ya maabara.
“Wananchi wanaishukuru Serikali yetu chini ya uongozi mzuri wa Rais D. Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kuchangia ujenzi na uboreshaji wa miundombinu ya elimu jimboni mwetu,” imesema taarifa hiyo.
Leave a comment