MAMLAKA ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA), imefuta ratiba za safari kwa mabasi 38 ya Kampuni ya New Force Enterprises kutokana na kile kilichoelezwa kuwa ni ajali za mara kwa mara. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na LATRA leo tarehe 3 Julai 2023, ratiba za safari za New Force zilizofutwa ni za kuanzia saa 9.00 alfajiri katika mabasi 10, na za kuanzia saa 11.00 alfajiri kwa mabasi 28.
Inadaiwa kuwa, uamuzi huo umekuja baada ya mabasi ya New Force, kupata ajali mara tano ndani ya mwezi mmoja, kati ya tarehe 6 Juni hadi 2 Julai, 2023.
Hata hivyo, LATRA imesema kuanzia tarehe 5 Julai 2023, mabasi hayo yatafanya safari zake kuanzia saa 12.00 asubuhi na kuendelea.
“Ni kwakuwa uchunguzi wa awali wa LATRA ulibaini kuwepo kwa uvunjaji wa makusudi wa kanuni, hususani kutumia ratiba za saa 9.00 alfajiri na saa 11.00 alfajiri , bila dereva kuwa amethibitishwa na LATRA na pengine dereva kuwa amethibitishwa lakini hatumii mfumo wa utambuzi wa dereva (i-button) anapoendesha basi,” imesema taarifa ya LATRA.
Taarifa ya LATRA imesema, kwa kuwa madereva wa mabasi hayo walivunja utaratibu kutotumia mfumo wa utambuzi wanapofanya safari, mamlaka hiyo imeshindwa kuwabaini kwa ajili ya kuwachukulia hatua za kisheria.
Jana Jumapili, basi la New Force lilipinduka katika Mlima Kitonga, huku chanzo kikidaiwa dereva kujaribu kulipita basi la mbele. Ajali hiyo imetokea zikiwa zimepita siku takribani 11, kwa basi lingine la kampuni hiyo kupinduka mkoani Njombe na kupoteza maisha ya watu watano.
Leave a comment