MAHAKAMA Kuu, Kanda ya Mbeya, imepanga kuanza kusikiliza mfululizo kesi ya kupinga mkataba wa ushirikiano wa kiserikali kati ya Serikali ya Tanzania na Serikali ya Dubai, kwa ajili ya uendeshaji bandari nchini, kuanzia tarehe 20 Julai 2023. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mbeya…(endelea).
Ratiba hiyo imepangwa leo Jumatatu, tarehe 3 Julai 2023 na Jaji Dustan Ndunguru,baada ya waleta maombi kupitia wakili wao, Boniface Mwabukusi, kuiomba mahakama iharakishe usikilizwaji wa maombi yao ya kuupinga mkataba huo, kwa madai kwamba unakiuka katiba ya nchi, pamoja na kutojali maslahi ya rasilimali za taifa.
Jaji Ndunguru amesema kesi hiyo itasikilizwa na jopo la majaji watatu, akiwemo yeye na wenzake, Jaji Mustafa Kambona na Abdi Kagomba.
Mbele ya Jaji Ndunguru, Wakili Mwabukusi aliitaka mahakama itoe amri ya kuzuia utekelezaji mkataba huo unaotarajiwa kufanywa na Tanzania kupitia Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) na Dubai kupitia kampuni ya DP World, hadi uamuzi wa kesi hiyo utakapotolewa.
Kesi hiyo Na. 5/2023, imefunguliwa na wanasheria wanne, akiwemo Alphonce Lusako na Emmanuel Chengula, dhidi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi na Bunge.
Wamefungua kesi kupinga mkataba huo, kwa madai kwamba kuna baadhi ya vipengele vyake vinakiuka katiba ya nchi.
Katika madai mengine, wanadai mkataba huo wa kimataifa umepelekwa bungeni kwa ajili ya kupitishwa bila kushirikisha umma na kutoa nafasi ya kutosha kwa wananchi kutoa maoni yao kinyjme cha Sheria ya Rasilimali za Taifa No. 5 ya 2017, kifungu cha 11 (1) na (2).
Wakili wa Serikali, Hangi Chang’a, ameiomba mahakama iwape muda zaidi kwa ajili ya kupitia hoja za waleta maombi kwa ajili ya kuzijibu.
Miongoni mwa hoja zilizoibuka kufuatia mkataba huo, ni muda wake wa utekelezaji, maslahi itakayopata nchi wakati wa utekelezwaji wake.
Leave a comment