MBUNGE wa Mlalo (CCM), Rashid Shangazi, ameishauri Serikali ipunguze kasi ya uzalishaji wahitimu katika taaluma ambazo nafasi za ajira zimepungua ikiwemo walimu, badala yake ilekeze nguvu kwenye kuzalisha wahitimu wa mafunzo ya ufundi stadi, ambao ni rahisi kujiajiri. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Shangazi ametoa maoni hayo leo tarehe 22 Aprili 2024, bungeni jijini Dodoma, akichangia hotuba ya makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji kwa mwaka wa fedha wa 2024/25, iliyowasilishwa na waziri wake, Prof. Kitila Mkumbo.
Mbunge huyo wa CCM amesema, sera ya elimu inapaswa kufanyiwa marekebisho ili iwe na mikakati ya kuzalisha watanzania ambao watakuja kuwa wazalishaji wazuri wa Taifa.
“Jambo mahususi nilitaka nishauri, bado tunazalisha sana watumishi katika kada ya walimu ambayo haiwezi kuajiri, vijana wengi wako mtaani hawajaajiriwa lakini bado vyuo vyetu vinaendelea kuzalisha walimu. Tunaomba wizara ilitizame hili jambo kwa upana kwamba kuna vyuo 35 vya Serikali vinazalisha walimu, je tuna umuhimu wa kuendelea kuwazalisha,” amesema Shangazi na kuongeza:
“Nadhani vizuri mipango ikatuelekeza tuwe na wanafunzi wengi kwenye vyuo vya aina ya DIT, huku tuwe na wanafunzi wengi ambao hata baadae hawatatusumbua kulazimika kuwatafutia ajira sababu watajiajiri wenyewe kulingana na maarifa watakayopata kupitia vyuo hivi.”
Leave a comment