KAMANDA wa polisi mkoa wa Songwe, Kamishna msaidizi wa Jeshi la polisi, Theopista Mallya amewaasa vijana kujiepusha na vitendo vya kihalifu ili kuishi kwa amani katika familia na jamii inayowazunguka. Anaripoti Ibrahim Yassin, Songwe…(endelea)
Pia ametoa wito kwa wananchi kutoa taarifa katika kituo chochote cha polisi pindi wanapobaini aina yoyote ya uhalifu ili kukomesha matukio ya kihalifu ikiwamo ubakaji ambao umekithiri katika siku za karibuni.
Kamanda Mallya ametoa wito huo jana tarehe 2 Julai 2023 katika Kanisa la Moravian ushirika wa Ebeneza Jimbo la Mbozi mtaa wa Majengo Mapya mkoani Songwe.
Amesema kupitia mpango maalumu wa utoaji elimu kwa jamii kuhusu kupinga masuala ya ukatili, Jeshi la Polisi limeamua pia kutumia majukwaa ya kidini ili kutokomeza vitendo hivyo ambavyo vinazidi kuididimiza jamii ya Watanzania.
Aidha, akitumia vifungu mbalimbali vya maandiko katika Biblia, Kamanda Mallya ameyataja baadhi ya madhara ya vitendo hivyo kuwa yanachangia ongezeko la matatizo ya akili, ulemavu, kujitenga na marafiki au familia, kifo na kufungwa jela.
“Vijana wanatakiwa kuwa wanatafakari pindi wafanyapo maamuzi yao ili kufanya maamuzi sahihi yatakayowaepusha na vitendo vya kiuhalifu,” amesema.
Kwa upande wa wachungaji wa kanisa hilo wakiongozwa na, Emmanuel Mgala ameahidi kuendeleza elimu hiyo kwa waumini na makanisani mengine ili jamii hiyo iachane na maisha ya kikatili na badala yake waishi kwa hofu ya Mungu.
Leave a comment