CHANZO cha vijana 21 waliopoteza maisha mwezi Juni huko nchini Afrika Kusini katika klabu moja ya usiku, imebainika kuwa ni sumu aina ya Methanol. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Kwa mujibu wa Naibu mratibu wa huduma za afya kwenye jimbo la Eastern Cape nchini humo, Daktari Litha Matinawe amesema kemikali hatari aina ya methanol huenda ilisababisha vifo vya vijana 21 waliokuwa wakisherehekea kumaliza mitihani yao ya elimu ya juu.
Kwa mujibu wa shirika la habari la AP, kemikali hiyo ilipatikana kwenye kila mwili wa waathirika hao baada ya kufanyiwa uchunguzi, wakati wataalam wakiendelea kubaini iwapo viwango vilivyopatikana vilitosha kusababisha vifo hivyo.
Vijana hao ambao wengi walikuwa wanafunzi walifariki wakati wakiwa ndani ya klabu kimoja cha usiku mjini humo.
Methanol ni kemikali yenye uwezo wa kulevya na ambayo hutumika kwenye viwanda au kutengeneza dawa za wadudu na wala sio pombe ya kutumiwa na wanadamu.
Vijana hao waliokuwa na umri kati ya miaka 13 na 17 walipatikana wakiwa wamekufa kwenye klabu hiyo, miili yao ikiwa imetapakaa kila mahali.
Polisi wa Afrika kusini wanasubiri matokeo kamili ya uchunguzi, ili kubaini ni nani atakaye funguliwa mashitaka kutokana na mkasa huo wenye kusikitisha.
Leave a comment