ALIYEKUWA Askofu Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri, Askofu Dk. Fredrick Shoo amewataka viongozi wa Chama cha ACT-Wazalendo kuendelea kupigania maslahi ya taifa kutokana na mshikamano waliouonesha. Anaripoti Faki Sosi, Kilimanjaro … (endelea).
Aidha, amewaonya viongozi hao wasikubali kuhongwa na kuwanyofoa kwenye mshikamano huo.
Askofu Dk. Shoo ametoa kauli hiyo leo Jumapili katika ibada iliyofanyika kwenye Kanisa la KKKT Dayosisi ya Kaskazini Usharika wa Nshara, Machame wilayani Hai mkoani Kilimanjaro.
Ibada hiyo imehudhuriwa pia na Kiongozi wa Chama cha ACT-Wazalendo, Dorothy Semu na kutoa shukrani kwa Mungu kutokana kheri na baraka anazozipata kwenye maisha yake ya kisiasa.
Viongozi wengine wa chama hicho waliofuatana na Dorothy ni pamoja na Zitto Kabwe – Kiongozi Mstaafu wa chama hicho, Isihaka Mchinjia – Makamu Mwenyekiti wa chama hicho Bara, Salim Biman – Katibu wa Itikadi na Uenezi na Janneth Fusi – Katibu wa Ngome ya Wanawake chama hicho.
Dk. Shoo amesema kuwa mshikamano wa viongozi hao katika kutetea wananchi ni ishara njemakwa Taifa.
“Kufika kwenu hapa kunaonesha mshikamano wenu katika kutete demokrasia na haki za watanzania. Msiangalie maslahi yenu binafsi endeleeni kutanguliza maslahi ya wananchi,” amesema Dk. Shoo.
Akitoa shukrani zake kanisani hapo, Dorothy amesema hatua zake zote alizopiga katika harakati za kisiasa ni baraka za Mungu.
Amesema miaka tisa aliyoingia kwenye siasa hakupanga kuwa kiongozi wa chama lakini baraka za Mungu zimemfanya kuwa kiongozi wa juu kabisa wa chama hicho.
Naye Mchungaji wa Kanisa hilo, Rodric Mlayi amesema kuwa Usharika huo unabahati kubwa kwa kupata viongozi wakubwa wawili wa kisiasa ambao ni Dorothy wa ACT na Freeman Mbowe Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).
Kwa upande wake Zitto Kabwe amewashukuru viongozi wa kanisa hilo na kuwaeleza kuwa ataendelea kumshika mkono kwa ushauri Dorothy ili kutekeleza wajibu wake kwa uweledi.
“Nataka nikuhakikishie Baba Askofu nitajitahidi kwa uwezo wangu kuhakikisha Dorothy anatimiza wajibu wake kwa usanifu,” amesema Zitto.
Leave a comment