MAHAKAMA nchini Tanzania imetoa wito kwa wadau wa mahakama kutumia mifumo ya Tehema ili kurahisha usikilizwaji wa mashauri na kuendana na kasi ya muhimili huo uliojipambanua kwenye matumizi ya Teknolojia. Anaripoti Faki Sosi, Morogoro … (endelea).
Hayo yamebainishwa leo tarehe 3 Aprili 2023 kwenye warsha ya mafunzo kwa waandishi wa habari za mahakama nchini yanayofanyika mkoani Morogoro yakilenga kuwapa uelewa wanahabari juu ya mwenendo wa mahakama kwenye matumizi ya Teknolojia ili kuwapa elimu wananchi.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa warsha hiyo Jaji Mfawidhi, Paul Ngwembe, amesema kuwa mahakama imepiga hatua kubwa kwenye matumizi ya Tehama kwa kumiliki mifumo mbalimbali inayowezesha kazi zake kirahisi.
“Nitoe wito kwa wenzetu ,Ofisi ya Mwendesha Mashtaka (DPP), Mawakili wa Serikali, na Mawakili wa kujitegemea kuiga mfano wa Mahakama katika masuala ya Teknolojia ili kusudi twende pamoja mahakama haiwezi kutekeleza majukumu yake ikiwa wadau muhimu wako nyuma tunataka na wananchi waijue vizuri mifumo hii ili waweze kuendesha mashauri yao bila gharama kubwa,” amesema Jaji Ngwembe.
“Mifumo hiyo ni pamoja mfumo wa Tanzania ambao huchapisha uamuzi, sheria na kanuni umefanya vizuri na kuifanya mahakama ya Tanzania kuwa ya kwanza Duniani kutembelewa na watu wengi kwa asilimia 82.7 ambapo nchi inayoifuta yenye mfumo kama huo ina asilimia 2.4,” amesema Jaji Ngwembe.
Amesema kuwa mfumo huo unaonyesha hukumu kwa uwazi pale ambapo inapotolewa pia unaonesha mashauri takribani 32 yanayoendelea duniani na kwamba ni mfumo rahisi kutumia na hauna gharama kubwa.
Jaji Ngwembe amesema kuwa Mfumo mwingine ni mfumo wa kieletroni wa kusajili mashauri na kesi mbalimbali bila kufika mahakamani na kusikilizwa.
“Tangu tumekuwa na mfumo huu tumerahisisha usikilizwaji wa mashauri huhitaji kufika mahakamani unaweza kufungua shauri kwa njia ya Tehama na shauri likasikilizwa mfumo huu unakwenda sambamba na mfumo usikizwaji wa kesi kwa njia ya video (Video Confrence)”amesema Jaji Ngwembe.
Jaji Ngwembe amesema Mfumo wa tatu unawasajili na kuwatambua mawakili wa mahakama, “umeleta matunda makubwa kwa mahakama umewezesha kutekeleza majukumu yake na kuwafichua mawakili vishoka ambapo walikuwa wanajifanya wanasheria, mahakimu au mawakili bila kuwa na sifa zinazowezesha kuwa mawakili, hivyo mfumo huo umepunguza kwa kwa kiasi kikubwa uhalifu wa kisheria”
Amesema kuwa sheria hamruhusu mtu asiye na sifa za kuwa wakili kufanya kazi ya uwakili na kwamba mwananchi kupitia mfumo huo atamtambua mtu mwenye sifa ya kufanya kazi ya uwakili kwa kuwa mfumo huo unaweka picha na jina la wakili anayestahili kufanya kazi.
Amesema kuwa mfumo wa nne unaowezesha mahakama kufanya kazi zake ni ule mfumo wa kusikiliza mashauri kwa njia ya video yaani Video Conference ambapo mfumo huo unanganisha Magereza, mahakama, wakili na Ofisi ya DDP .
“Mfumo huu unaweza kusiliza shauri bila kufika mahakamani mimi nimesikiliza mashauli na mashahidi kutoka Kigoma, Mtwara, au Sumbawanga nikiwa hapa Morogoro shahidi anatoa ushahidi wake mpaka anamaliza na tunamuuliza maswali mpaka tunamaliza, mfumo huu wananchi wakiuelewa vizuri kutasaidia kupunguza gharama za kuendesha mashauri ” amesema Jaji Ngwembe.
Amesema kuwa Mahakama haijaishia hapo imeongeza ufanisi wa utoaji elimu ya sheria kwa wananchi kwa kuanzisha kituo cha kupokea simu za wananchi ili kuwafahamisha masuala mbalimbali ya kisheria.
Leave a comment