WATU 10 wanadaiwa kupoteza maisha baada ya lori lililokuwa likisafirisha changarawe kupoteza mwelekeo na kuparamia kijiwe cha bodaboda katika eneo lao mjini Migori nchini Kenya. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa…(endelea).
Waliopoteza maisha katika ajali hiyo iliyotokea leo tarehe 8 Aprili 2023, inaelezwa ni vijana wa bodaboda waliokuwa wakisubiria wateja kwenye kijiwe chao.
Umati mkubwa wa watu ulimiminika eneo la tukio ili kuwanusuru majeruhi na kuwakimbiza hospitalini kwa matibabu.
Kwa mujibu wa raia mmoja aliyeshuhudia na kuzungumza na runinga ya TV47, breki za lori hilo zilifeli na kuingia katika kundi hilo la bodaboda ambao walikuwa wanasubiri abiria.
Ajali hiyo imetokea karibu na shule ya msingi ya Migori. Eneo la tukio lilikuwa limejaa damu na miili. Vyuma pia vilikuwa vimetapakaa eneo hilo.
Eneo la tukio linaripotiwa kuwa na zaidi ya miili 10 huku gari za kubeba wagonjwa ‘ambulansi’ na zima moto kutoka kwa serikali ya kaunti ya Migori zikifika eneo la ajali hiyo.
Leave a comment