WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Hamadi Masauni amesema upo umuhimu wa kutenganisha shughuli za msingi za magereza na zile shughuli za kibiashara. Anaripoti Juliana Assenga, UDSM …. (endelea).
Waziri huyo ameyasema hayo leo tarehe 29 Agosti, 2022 katika hafla ya kuapishwa kwa aliyekuwa Kaimu Kamishna wa Magereza Huduma za Urekebu, Ramadhani Nyamka kuwa Generali Kamishna wa magereza, iliyofanyika Ikulu ya Chamwino Dodoma.
Waziri amesema yapo madhara yaliyokwisha shuhudiwa kwa kushindwa kutenganisha shughuli za msingi na shughuli za kibiashara katika magereza ikiwemo kushindwa kurekebisha tabia za wafungwa na wanaporudi mtaani kuendelea na vitendo vya uhalifu.
Waziri ameendelea kusema madhara mengine ni pamoja na kutokuwepo na utaratibu mzuri katika utumiaji wa rasimali za magereza na hata kupelekea kutokuwa na maboresho na maendeleo katika magereza nchini.
Wakati huohuo Waziri wa Katiba na Sheria, Dk. Damas Ndumbaro, amewapongeza majaji na Kamishna Jenerali wa Magereza kwa kuaminiwa na kuteuliwa na kuwasihi kuzingatia katiba na sheria za Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania katika kutenda haki kwa wananchi wote.
Waziri huyo ametoa pongezi zake kwa Rais Samia kwa mchango wake katika kuleta maendeleo ndani ya magereza, pamoja na kutenga kiasi cha fedha kwa ajili ya kukamilisha miundombinu za mahakama na kuhamasisha utendaji kwa mahakama.
Ndumbaro amempongeza Jaji Mkuu Profesa Ibrahimu Juma kwa namna anavyoweza kuiendesha shughuli zote za mahakama na kuweza kufanya maboresho makubwa.
Leave a comment