Kiongozi wa chama kikuu cha upinzani nchini Zimbabwe, Nelson Chamisa ametangaza kujiuzulu wadhifa wake na uanachama wa Chama cha Citizens Coalition for Change (CCC),
Hatua hiyo inajiri ikiwa ni miezi michache baada ya kushindwa katika uchaguzi mkuu wa rais, akilalamikia vitisho na ghasia zinazofanywa na utawala. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa … (endelea).
Katika taarifa yake aliyoitoa jana Alhamis, Chamisa (45) alisema, “Ninawaarifu wananchi wenzangu wa Zimbabwe na dunia kwamba, kuanzia sasa hivi, mimi sijihusishi tena na CCC.
“Wazo msingi la CCC limehujumiwa, limeshushwa hadhi, limeporwa na ZANU-PF kupitia unyanyasaji na taasisi za Taifa,” amesema, akikishutumu chama tawala cha rais Emmerson Mnangagwa kwa kuwa na mbinu chafu.
Uamuzi huo wa kushangaza umetolewa baada ya Mnangagwa (81) kushinda mhula wa pili katika uchaguzi wa rais, na kumshinda Chamisa katika uchaguzi ambao pia umekipa chama tawala cha ZANU-PF idadi kubwa ya wabunge.
Wafuatiliaji wa uchaguzi wa kimataifa wamesema upigaji kura haukuwa na viwango vya kidemokrasia, na mivutano ya kisiasa imeongezeka tangu wakati huo.
Akijulikana kwa jina la “Mamba” Mnangagwa aliingia madarakani kwa mara ya kwanza baada ya mapinduzi yaliyomuondoa madarakani kiongozi mkongwe Robert Mugabe mwaka 2017.
Chamisa alionekana akilitumia jina la utani la Mnangagwa, akitangaza: “Nimekataa kuogelea mtoni na mamba mwenye njaa. Tunataka kujiondoa kutoka kwa wanasiasa wadanganyifu”
Kwa muda mrefu chama cha ZANU-PF kimekuwa kikishtumiwa kwa kutumia mahakama kuwalenga wapinzani wa kisasa na kuwanyamazisha.
Chama cha ZANU-PF kimepata viti 177 kati ya 280 katika bunge la taifa wakati chama CCC kimepata viti 104 baada ya uchaguzi huo wa tarehe 23 Agosti 2023.
Leave a comment