WAKILI wa Halima Mdee na wenzake, Edson Kilatu, amesema wako katika hatua za mwisho za kufungua kesi ya wabunge hao viti maalum, kupinga mchakato uliotumiwa na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kuwafukuza uanachama. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Wakili Kilatu ametoa kauli hiyo leo Jumanne, tarehe 19 Julai 2022, akizungumza na MwanaHALISI Online, kuhusu hatua waliyofikia katika ufunguaji wa kesi hiyo.
“Tupo hatua za mwisho kufungua. Tukifungua tutakujulisha. Ahsante,” amesema Wakili Kilatu, alipokuwa anazungumza na MwanaHALISI Online.
Mahakama Kuu, Masjala Kuu ya Dar es Salaam, tarehe 8 Julai 2022, iliwapa siku 14 wabunge hao viti maalum 19, baada ya kukubali maombi yao ya kupata kibali cha kufungua kesi dhidi ya Chadema, ili kupinga mchakato wake uliotumika kuwavua uanachama, wakidai haukuwa halali.
Katika maombi yao, Mdee na wenzake 18, wanaiomba mahakama ifanye mapitio ya kimahakama, dhidi ya mchakato uliotumiwa na Chadema kuwafukuza ndani ya chama hicho, wakidai haukufuata sheria kwa kuwa hawakupewa nafasi ya kujieleza na ulikuwa wa upendeleo.
Mbali na Mdee, wabunge wengine viti maalum wanaopinga kufukuzwa Chadema, ni Jesca Kishoa, Ester Bulaya, Esther Matiko, Hawa Mwaifunga, Grace Tendega, Agnesta Lambart, Cecilia Pareso, Asia Mwadin Mohamed na Felister Njau.
Wengine ni, Naghenjwa Kaboyoka, Sophia Mwakagenda, Kunti Majala, Styella Siyao, Salome Makamba, Anatropia Theonest na Conchesta Lwamlaza.
Wabunge hao walivuliwa uanachama wa Chadema, tarehe 27 Novemba 2020, ambapo walikata rufaa katika Baraza Kuu la chama hicho, ambazo zilitupiliwa mbali Mei 2022.
Baada ya rufaa hizo kutupwa, Mdee na wenzake 18, walikwenda mahakamani kufungua maombi ya kupinga kuvuliwa uanachama.
Leave a comment