WANAHABARI nchini wametakiwa kuandika habari zikiwemo za uchaguzi kwa kuzingatia maadili, sheria na kanuni ili kuepuka vichocheo vya machafuko nchini na duniani kwa ujumla. Anaripoti Christina Haule, Morogoro … (endelea).
Mkufunzi wa masuala ya habari kutoka Mtandao wa redio za kijamii Tanzania (TADIO), Rose Haji alisema hayo jana wakati akiongea na mameneja wa redio 35 nchini waliokuwa wakipewa mafunzo ya kuripoti habari bila migongano yaliyofadhiliwa na UNESCO kupitia mradi wa SDC na kufanyika mjini hapa.
Alisema wanahabari wanapaswa kutumia vizuri kalamu zao ili kufikia hatua nzuri katika kuelimisha na kuburudisha jamii na kwamba kinyume na hapo anaweza kufikishwa mahakamani huku chombo chake cha habari kikifungiwa.
Rose alisema kwa kufuata taaluma inavyotaka na kuzingatia maadili mwandishi anapaswa kuandika habari kwa kulichambua tatizo na sio kuandika tatizo lililopo tu jambo litakaleta shida nyingine.
Alisema kama chombo cha habari kinayonafasi ya kuangalia namna ya kumaliza tatizo kwa kuandika ukweli kwa kuzingatia mila, tamaduni na dini zilizopo ili kuepuka migogoro kwa sababu wanahabari wanayo nafasi kubwa ya kumaliza tatizo na kulikuza tatizo.
“Wakati mwingine kuna migogoro mahala pa kazi lakini kwa kuzingatia sheria za kazi zilizopo wanahabari wanapaswa kuangalia kuwa na usawa wa vipindi kwa kushirikisha wahusika wote ili kuondoa migogoro,” alisema Rose.
Hata hivyo alisema wanahabari wanapaswa kuandika habari wakijikita katika uelimisha kupitia sheria za haki za binadamu ili kuepuka migogoro ya kijamii ambayo huleta uvunjifu wa amani katika nchi yoyote.
Hivyo aliwashauri wanahabari kuhakikisha wanazijua vizuri sheria za haki za binadamu ili waweze kuwa waandishi wazuri wa habari za kijamii kwa kuzingatia hekima, busara umahiri na weredi.
Naye Mratibu wa TADIO, Cosmas Lupoja alisema lengo la semina hiyo ni kuwawezesha mameneja kuzijua sheria za vyombo vya habari na kuzisimamia ili kuepuka kutoa habari zenye migogoro na kuhakikisha haziendi hewani au kwenye vyombo vya habari.
Lupoja alisema lengo la TADIO ni kusaidia jamii hasa ya maeneo ya vijijini kukua katika kutoa taarifa zenye ukweli ili kuleta maendeleo.
Leave a comment