MKURUGENZI mkuu wa kampuni ya Wasafi Naseeb Abdul maarufu kama ‘Diamond Platnumz’ ametangaza ujio wa tamasha kubwa la burudani Wasafi Festival ambalo linatarajia kuanzia mkoani Mtwara 24 Novemba, 2018 na kuzunguza katika baadhi ya mikoa nchini na kuelekea mpaka n je ya nchi. Anaripoti Kelvin Mwaipungu … (endelea).
Tamasha hilo lenye kauli mbiu ya ‘Mchezo usiuchezee wewe Kabisa’ litafanyika mkoani Mtwara katika Uwanja wa Nangwanda Sijaona, na baadae kwenda mkoani Iringa na Morogoro na baadae kwenda kufanyika nchini Kenya katika jiji la Nairobi 31 Novemba Mwaka huu.
Akizungumza mbele ya waandishi wa habari Diamond alisema kuwa mbali na burudani ujio wa tamasha hili utakwenda sambamba na kusaidia jamii katika mkoa husika kama kutoa mitaji kwa wakina Mama 200 pamoja na kusaidia wanafunzi.
“Tunataka tamasha hili kila linapofika liwanufaishe wakazi wa pale siyo kwenda tu kuchukua hela zao na kusepa, na kwa kuanzia tutawasaidia kina mama,” alisema Diamond.
Sambamba na hayo Diamond aliongezea kuwa tamasha hilo litajumuisha wasanii wote wanaofanya vizuri nchini kwa sasa na huku akitamani hata msanii mwenake ambaye anaonekana kuwa mpinzani wake mkubwa katika kazi zao za muziki Ali Kiba naye akiwepo.
“Natamani kaka yangu Ali Kiba naye awepo na ninaamini uongozi wangu utaanza mazungumzo naye na huko alipo kama anafuatilia wasafi ajue tungehitaji uwepo wake, kwani inabidi tutoke kwenye muziki wa mabifu na tuingie katika kutengeneza hela na kuisaidia jamii inayotuzunguka,” aliongeza Diamond.
Leave a comment