TUME ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) imetangaza kuwa na mfumo mpya wa kielektroniki utakomwezesha mwanafunzi kuthibitisha chuo anachokwenda kusoma baada ya kuchaguliwa na zaidi ya chuo kimoja. Anaripoti Khalifa Abdallah … (endelea).
Akizungumza na waandishi wa habari Katibu Mtendaji TCU, Charles Kihampa amesema kutokana na kuwepo kwa malalakimiko TCU imeamua kutoa code maalumu ya siri kwa wanafunzi watakaochaguliwa na zaidi ya chuo kimoja itakayomwezesha kuthibitisha chuo au program anayotaka kusoma.
Kihampa amesema kuwa TCU itatuma SMS yenye namba hiyo maalumu ya siri ambayo itakuwa ni siti ya mwombaji pekee na atatakiwa kuitoa pale tu anapotaka kuthibitisha chuo anachotaka kusoma.
Amesema tume itatoa muda maalumu kwa waombaji kuthibitisha chuo au programu ya masomo anayopenda.
Hata hivyo hivi karibuni Mwenyekiti wa Mtandao wa Wanafunzi Tanzania (TSNP), Abdul Nondo amekuwa akisisitiza kuwa Tume hiyo iunde utaratibu maalamu kwa ajili ya wanafunzi kuweza kuthibitisha vyuo wanavyotaka kwenda kutokana na mkanganyiko uliokuwepo.
Nondo alisema kuwa baadhi ya vyuo vimekuwa na utaratibu wa kuwakubalia wanafunzi kuwa wamethibitisha kusoma katika vyuo vyao hata kama hawajathibitisha hivyo pindi wanapochaguliwa na vyuo zaidi ya kimoja jambo ambalo husababisha wanafunzi hao kukosa hata mikopo.
Katika hatua nyingine TCU imetangaza kufunga dirisha la maombi ya kujiunga na masomo ya shahada ya kwanza katika vyuo vikuu na taasisi za elimu ya juu la awamu ya kwanza ambalo liliansa Julai 20, 2018 ifikapo kesho tarehe 15 Agosti, 2018.
“Baada ya kufunga dirisha la udahili urodha ya waombaji itaidhinishwa na orodha ya seneti au bodi za kitaaluma zitawasilishwa TCU ili kuhakiki kama wahusika wanakidhi vigezo na baada ya TCU kuchagua orodha ya waombaji itawasilisha waombaji wenye sifa za kujiunga na vyuo,” amesema Kihampa.
Leave a comment