MISAADA ya kiusalama kwa Pakistan yenye thamani ya takriban dola milioni 900 itasitishwa hadi pale Pakistan itakapochukua hatua madhubuti ya kupambana na kundi la wanamgambo wa Afghanistan la Taliban na la Haqqani.
Hatua hiyo ilitangazwa na Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani huku ikisema Rais Donald Trump amekerwa na Pakistan kushindwa kuchukua hatua za kutosha dhidi ya makundi hayo mawili ambayo yamekuwa yakiitumia nchi hiyo kama sehemu ya kujificha na kufanya mashambulizi katika nchi jirani ya Afghanistan.
Ufadhili huo utakaositishwa utaathiri ununuzi wa vifaa vya kijeshi, mafunzo, huduma nyingine za kijeshi na mpango wa kupambana na ugaidi.
Akiwahutubia wanahabari, Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje wa Marekani, Heather Nauert amesema hatua hiyo ya kusitisha ufadhili, haitaathiri misaada inayotolewa kwa raia wala ile ya kusaidiai uchumi wa Pakistan.
Nauert amesema fedha hizo huenda zikaidhinishwa kutolewa iwapo Pakistan itachukua hatua zinazostahili kukabiliana na makundi ya kigaidi.
Bunge la Marekani limefahamishwa kuhusu uamuzi huo wa kustishia misaada kwa Pakistan.
Pakistan kwa muda mrefu imekanusha shutuma kuwa imeshindwa kupambanana na makundi ya wanamgambo yanayopambana dhidii ya majeshi ya Afghanistan na ya kigeni kutokea upande wa pili wa mpaka.
Leave a comment