MTANDAO wa kupinga utumikishwaji watoto Tanzania, umeiomba Serikali iweke mikakati itakayosaidia kutokomeza ajira za watoto ili kulinda ustawi wao. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Wito wa mtandao huo umetolewa leo tarehe 12 Juni 2023, jijini Dar es Salaam, wakati wa maadhimisho ya siku ya kimataifa ya kupinga utumikwaji watoto.
Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi ya mtandao huo, Samatta Ibrahim, amesema licha ya Serikali kuweka sheria zinazolinda haki za watoto, bado changamoto ya utumikishwaji ipo, hivyo inatakiwa kuanza kuwabaini wanaotekeleza vitendo hivyo kwa ajili ya kuwachukulia hatua.
Samatta amesema sekta zinazoongoza kwa kuwatumikisha watoto ni madini, kilimo, uvuvi na shughuli za majumbani.
Katika hatua nyingine, Samatta amesema changamoto hiyo inatokana na sababu mbalimbali, hususan ya hali duni ya maisha kitendo kinachopelekea familia kuwaagiza watoto wakafanye kazi kwa ajili ya kujipatia ridhiki.
Amesema ili changamoto hiyo itafutiwe ufumbuzi, Serikali inapaswa kuongeza juhudi za kuwakomboa wananchi kiuchumi hasa wa vijijini ili waweze kutunza familia zao.
Mjumbe wa mtandao huo, Eddna Chandeu, amesema kwa mujibu wa takwimu za 2020, Tanzania Ina watoto milioni 4.2 wanaotumikishwa hasa kutoka maeneo ya vijijini.
Kwa upande wake Afisa Ustawi wa Jamii kutoka Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam, Joyce Maketa, amesema Idara ya ustawi wa Jamii imekuwa ikichukua hatua mbalimbali kuwasaidia watoto wanaobainika kutumikishwa ikiwemo kuwarejesha katika familia zao.
Leave a comment