Sunday , 19 May 2024
Home Kitengo Habari Kimataifa Mbivu, mbichi urais wa Ramaphosa mwezi huu
KimataifaMakala & Uchambuzi

Mbivu, mbichi urais wa Ramaphosa mwezi huu

Rais Cyril Ramaphosa
Spread the love

MWISHONI mwa mwezi huu, raia wa Afrika Kusini watapiga kura katika uchaguzi mkuu ambao unaweza kuleta mabadiliko makubwa zaidi ya kisiasa katika miongo mitatu, huku chama tawala cha African National Congress (ANC) kikiwa katika hatari ya kupoteza wingi wake wa wabunge. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa… (endelea).

Zaidi ya watu milioni 27 wameandikishwa kwenye daftari la wapiga kura kwa ajili ya kushiriki kupiga kura tarehe 29 Mei kuchagua bunge jipya. Bunge zima la Afrika Kusini lenye viti 400 ndilo litamchagua rais.

Baada ya kuongoza vita dhidi ya utawala wa watu weupe walio wachache, chama cha shujaa aliyepinga ubaguzi wa rangi Nelson Mandela kimekuwa kikishinda kwa zaidi ya asilimia 50 ya kura katika kila uchaguzi wa kitaifa tangu uchaguzi wa kwanza wa kidemokrasia mwaka 1994.

Hata hivyo hali imebadilika kiasi kwamba chama hicho kinakabiliwa na kukatishwa tamaa na utawala wake, ambao wakosoaji wanasema kimeshindwa kutekeleza ahadi zake nyingi.

Jumamosi iliyopita, Rais Cyril Ramaphosa, 71, alitetea rekodi ya ANC, akisema Afrika Kusini leo ni “mahali pazuri zaidi kuliko ilivyokuwa miaka 30 iliyopita”.

Aliorodhesha maendeleo katika usawa na upatikanaji wa elimu, mageuzi ya ardhi yenye lengo la kukabiliana na tofauti za rangi na ujenzi wa nyumba na hospitali.

Lakini ukosefu wa ajira uko katika asilimia 32, viwango vya uhalifu vimesalia kuwa juu sana na miundombinu inayoharibika – kuanzia reli na barabara hadi bandari na vituo vya umeme – inadhoofisha uchumi wa kiviwanda zaidi wa Afrika.

Watu milioni 62 nchini humo wanakabiliwa na matatizo ya mara kwa mara ya maji na kukatika kwa umeme.

Nelson Mandela

Pengo kati ya walionacho na wasionacho ndilo kubwa zaidi duniani, kulingana na Benki ya Dunia.

Msururu wa kashfa za ufisadi umezidi kuumiza chama tawala, ambacho kilishuka chini ya asilimia 50 kwa mara ya kwanza katika uchaguzi wa mitaa wa 2021.

Kura ya maoni

Kura ya maoni iliyoandaliwa na shirika la Ipsos ambayo matokeo yake yalitangazwa wiki iliyopita ilionesha uungwaji mkono kwa ANC ulikuwa juu kidogo ya asilimia 40. Katika uchaguzi mkuu uliopita wa 2019, ilishinda zaidi ya asilimia 57.

Iwapo kitapoteza wingi wake kamili bungeni, chama hicho kitalazimika kutafuta washirika wa muungano ili kubaki madarakani.

Jacob Zuma

Chama kikubwa zaidi cha upinzani, cha kiliberali cha Democratic Alliance (DA), kimefikia makubaliano na takriban vyama 10 vidogo.

Hata hivyo, pamoja na vyama hivyo kushirikiana, bado wingi wao hautoshi kuiangusha ANC.

Utafiti wa Ipsos uliiweka DA, ambayo kwa muda mrefu imekuwa ikijitahidi kufuta dhana kwamba inawakilisha wazungu wachache, kwa karibu asilimia 22.

Msukosuko mkubwa zaidi wa uchaguzi unaweza kutoka chama kipya cha rais wa zamani Jacob Zuma, 82.

Mkongwe huyo wa ANC aliyechukizwa na uongozi wa chama chake cha zamani amezindua chama kilichojitenga, uMkhonto we Sizwe (MK), ambacho kinatishia kugawanya kwa kiasi kikubwa sehemu ya kura za chama tawala.

Akiwa amelazimishwa kuondoka ofisini chini ya wingu la ufisadi, Zuma mwenye nguvu bado anafurahia kuungwa mkono na watu wengi, hasa kutoka jimbo la nyumbani la KwaZulu-Natal.

Ikipewa jina la mrengo wa kijeshi wa ANC wakati wa mapambano dhidi ya ubaguzi wa rangi, MK haikujulikana kivitendo miezi michache iliyopita, lakini Ipsos ilikadiria uungwaji mkono wake wiki iliyopita kwa asilimia 8.4.

ANC haijafanikiwa kujaribu kukiondoa chama kipya na kukizuia kutumia jina la MK, kwa madai ya wizi wa mali miliki.

Uwezo wa Zuma kugombea mwenyewe umepingwa kutokana na kutiwa hatiani 2021 kwa kudharau mahakama.

Mahakama ya Kikatiba bado haijatoa uamuzi juu ya kesi hiyo ya kiongozi wa zamani anayeshutumiwa kwa ufisadi kwa sasa bado anapiga kura. Baadhi ya viongozi wa MK wameonya huenda ghasia zikazuka iwapo Zuma atazuiliwa.

Zaidi ya watu 350 waliuawa mwaka 2021 katika maandamano, ghasia na uporaji uliochochewa na kufungwa kwa Zuma, ambaye alikataa kutoa ushahidi kwa jopo lililochunguza ufisadi wa kifedha na urafiki wakati wa urais wake wa 2009-2018.

Zuma aliachiliwa kwa msamaha wa matibabu miezi miwili tu baada ya muhula wake. “Ni kama tayari tumeshinda,” aliuambia umati wa wafuasi walioshangilia katika mji aliozaliwa wa Nkandla wiki iliyopita.

Matokeo yanapaswa kutangazwa ndani ya siku tatu baada ya kupiga kura.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za SiasaKimataifa

Bunge kumuweka katibu mkuu wa EAC kikaangoni

Spread the loveAliyekuwa Katibu mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki Dk. Peter...

Makala & UchambuziTangulizi

Askofu Bagonza: Potofu huzaa potoshi/ potoshi huzaa potofu?

Spread the loveDayosisi 7 za KKKT katika kanda ya Ziwa na Magharibi,...

Kimataifa

Palestina mwanachama wa 194 wa UN

Spread the loveBaraza Kuu la Umoja wa Mataifa jana Ijumaa limepitisha kwa...

Habari za SiasaMakala & Uchambuzi

Rais Samia ni Mzanzibari: Shida Iko Wapi?

Spread the loveTAIFA linakabiliwa na upungufu wa fikra sahihi. Upungufu huu unaonekana...

error: Content is protected !!