MAHAKAMA Kuu ya Tanzania, Masjala Kuu jijini Dar es Salaam, imeamua kwamba, ni haki ya kibinadamu kwa mwananchi kutumia mtandao wa Club House, pasipo kutumia mtandao binafsi wa kidigitali (VPN) unaosaidia mtu kutumia mtandao wa kijamii uliofungiwa, pasipo mamlaka husika kubaini. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Uamuzi huo ulitolewa na mahakama hiyo tarehe 3 Mei 2024, mbele ya majaji, Dk. Ubena Agatho na Dk. Angelo Rumisha, katika kesi ya madai Na. 27860/2024, iliyofunguliwa na Mkuu wa Idara ya Utetezi wa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu (THRDC), Paul Kisabo, dhidi ya Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) na Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG).
Mahakama hiyo iliamua kwamba, mwananchi ana haki ya kufikia mtandao wa Club House ambao ulikuwa unatumiwa na makundi mbalimbali kufanya mijadala, pasipo kuwekewa vizuizi vyovyote kinyume cha sheria, kwani ana haki ya kupata uhuru bila vikwazo kwa mujibu wa Ibara ya 30 (2) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Wakili Kisabo alifungua kesi hiyo akiiomba mahakama itamke kwamba zuio dhidi ya matumizi ya mtandao huo linalodaiwa kuwekwa na TCRA tangu Agosti 2023 hadi sasa, ni kinyume cha katiba ya nchi, mikataba ya kimataifa ya haki za binadamu na sheria za ndani.
Pia, aliiomba mahakama iiamrishe TCRA ifungue mtandao wa Club House ili wananchi wapate fursa ya kuutumia pasipo kutumia VPN, ambayo kwa mujibu wa mamlaka hiyo ni kinyume cha sheria kutumia programu hiyo fiche pasipo kupewa kibali.
Leave a comment