BALOZI mpya wa Urusi nchini Tanzania, Andrei Avetisyan, amesema nchi yake imejipanga kuja na mikakati ya kuimarisha uhusiano na ushawishi wake katika mataifa ya Afrika, hususani ya kibiashara na uwekezaji. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Balozi Avetisyan ametoa kauli hiyo leo Jumanne, tarehe 28 Juni 2022, akielezea hatua ambazo Urusi inazichukua kuzisaidia nchi za Afrika, kukabiliana na athari zilizotokana na mzozo uliobuka kati yake na Ukraine.
Miongoni mwa athari hizo ni kupanda kwa bei ya mafuta, gesi, ngano na mbolea.
Balozi Avetisyan amesema, Urusi ilikuwepo Afrika, lakini awamu hii inakuja kwa uzito wa kipekee.
“Ssasa tunakuja Afrika, sijasema kwamba tunarudi sababu hatujawahi kuondoka. Lakini tunakuja serious (kwa uzito),” amesema Balozi Avetisyan.
Akizungumzia athari zinazotokana na mzozo kati ya Urusi na Ukraine, Balozi Avetisyan amesema nchi yake itaendelea kutoa ushirikiano kwa mataifa ya Afrika, Asia na mengine duniani.
Licha ya vikwazo vya kiuchumi na usafirishaji walivyowekewa na jumuiya za kimataifa kufuatia operesheni yake ya kijeshi nchini Ukraine.
Amesema nchi yake iko tayari kutoa msaada wa chakula, mafuta, mbolea pamoja na gesi kwa nchi za Afrika, ikiwemo Tanzania.
“Kwa sasa tunaangalia nchi za Asia na Afrika, tunahitaji nafasi ya kuwa makini katika kuimarisha uhusiano wa biashara na uchumi na mataifa mengine,” amesema Balozi Avetisyan.
Akizungumzia mahusiano ya Urusi na Tanzania, Balozi Avetisyan amesema yanaendelea kuimarika na kwamba atakuwa balozi mzuri katika kuhakikisha ndoto za Rais Samia Suluhu Hassan, za wawekezaji wa kigeni kuja nchini, zinatimia.
“Mahusiano kati ya Urusi na Tanzania yako vizuri, na nitatafsiri ujumbe wa Rais Samia kwa wekezaji wa kigeni kwa wawekekzaji wa Urusi kwa kuwaambia Tanzania ni salama kwa uwekezaji na kufanya biashara. Naamini kwa kushirikiana pamoja tutasaidia upatikanaji wa mbolea sababu mnajua Urusi ndiyo mzalishaji mkuu wa mbolea na tutaongeza uzalishaji,”
Aidha, Balozi Avetisian amesema, hivi karibuni Tanzania na Urusi zitasaini makubaliano ya ushirikiano ikiwemo kuanzisha tume itakayoshughulikia mahusiano kati ya mafia hayo mawili ikiwemo biashara kwa maslahi ya pande zote mbili.
Leave a comment