Uongozi mpya wa kijeshi nchini Niger umeituhumu Ufaransa kutaka kuingilia kati kijeshi ili kumrejesha madarakani Rais aliyeng’olewa Mohammed Bazoum. Anaripoti Mariam Mudhihiri kwa msaada wa Mitandao ya Kimataifa…(endelea).
Hayo yanajiri wakati mivutano ikiongezeka kati ya Niger na Ufaransa, iliyokuwa mtawala wa kikoloni kwa Niger, na majirani zake.
Aidha, Waziri wa mambo ya nje wa Ufaransa, Catherine Colonna amekanusha madai hayo jana Jumatatu jioni na kuongeza kuwa bado upo uwezekano wa kumrejesha madarakani Bazoum.
Kutokana na madai hayo, Serikali za Mali na Burkina Faso zinazoongozwa na wanajeshi nazo zilionya kwamba uingiliaji kati wowote wa kijeshi nchini Niger utachukuliwa pia kama tangazo la vita kwa nchi zao zote mbili.
Bazoum ambaye ni mshirika wa karibu wa nchi za magharibi ambaye kuchaguliwa kwake miaka miwili iliyopita kuliashiria kukabidhiana madaraka kwa njia ya amani kwa mara ya kwanza tangu uhuru wa Niger, aliondolewa madarakani tarehe 26 Julai na kiongozi wa kikosi cha ulinzi wa rais.
Mkuu huyo wa kikosi cha ulinzi wa rais, Jenerali Abdourahamane Tiani alijitangaza kuwa kiongozi, lakini madai yake yalilaaniwa kimataifa na Jumuia ya uchumi ya nchi za Afrika magharibi (ECOWAS) ambayo ilimpa wiki moja kurudisha madaraka.
Leave a comment