KAMPENI ya kuitangaza bandari ya Dar es Salaam kimataifa imetajwa kuanza kuzaa matunda baada ya wafanyabiashara na wakazi wa Zimbabwe kuichagua bandari hiyo kupitisha mizigo mbalimbali hususani magari. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Hatua hiyo imetajwa kuendelea kuvutia wateja wengi wa kimataifa kuitumia bandari ya Dar es Salaam na kuilazimu Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) kufungua ofisi katika jiji la Harare ili kurahisisha utoaji huduma kwa wateja wake.
Hayo yamebainishwa wiki iliyopita na Afisa Uhusiano Mkuu wa Mamlaka ya Bandari Tanzania, Levina Kato wakati akiwasilisha mada kwenye Mkutano Mkuu wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) uliofanyika mkoani Lindi.
Kati alisema mbali na kampeni iliyofanywa na mamlaka hiyo, baada ya nchi jirani ikiwamo Afrika Kusini ambako Zimbabwe walikuwa wanatumia kupitisha magari yao, wamepitisha sheria ambazo zinaongeza gharama kwa waagizaji magari.
“Walipitisha sheria ya kuzuia magari hayo mapya yasipitishwe kwenye barabara zao hivyo wateja wakawa wanatumia gharama kusafirisha mzigo kupitia car carrier kwa sababu lazima anayepakia magari alipwe.
“Kwa kuwa ni gharama kubwa kwao, wakaamua kuchagua bandari za Tanzania ili wayaendeshe wenyewe magari hayo badala ya kupitia Afrika Kusini na Zambia,” alisema.
Aidha, aliongeza kuwa TPA imeendelea kuboresha bandari mbalimbali nchini ikiwamo Lindi ambako sasa mkandarasi yupo ‘site’ kuboresha bandari ya uvuvi.
Mbali na maboresho hayo kwenda sambamba na bandari ya Mtwara, Kato alisema kwa upande wa Mwanza mamlaka hiyo inaboresha bandari za mkoa huo ili ziweze kuhudumia vema sokola Uganda kupitia eneo maarufu la biashara Port Bell.
Leave a comment