KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu, imeitaka Serikali kuimarisha usimamizi katika miradi ya maendeleo ya kimkakati ya uchukuzi ikiwemo barabara na reli, ili kuhakikisha inatekelezwa kwa ufanisi na thamani ya fedha iwepo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Wito wa kamati hiyo umetolewa bungeni jijini Dodoma leo Jumatatu na mwenyekiti wake, Seleman Kakoso, akiwasilisha maoni ya kamati yake kuhusu makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Uchukuzi, kwa mwaka wa fedha wa 2024/25.
Aidha, Kakoso amesema kamati hiyo inaishauri serikali kuongeza ubunifu katika ukusanyaji mapato yatokanayo na miradi ya uchukuzi, ili yaongezeke.
“Kamati imeshuhudia kwa sehemu kubwa miradi ya kimkakati ambayo ilianza kutekelezwa katika serikali ya awamu ya tano, serikali ya awamu ya sita imetekelezwa kwa ufanisi. Kwa mkuktadha huo na kwa kuthamini mtaji wa fedha za maendeleo zinatokana na kodi za wananchi, kamati inaishauri serikali kuongeza ufanisi na ubunifu katika utekelezaji wa miradi hiyo,” amesema Kakoso na kuongeza:
“Tunaishauri Serikali kusimamia kikamilifu utekelezaji wa miradi yake yote ili iweze kuakisi viwango bora endelevu na kuwepo kwa thamani ya fedha.”
Miongoni mwa miradi ya mkakati ya miundombinu ambayo ilianza kutekelezwa katika Serikali ya Awamu ya Tano na kuendelezwa na Serikali ya Awamu ya Sita, ni ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR) na miradi ya barabara.
Leave a comment