Tanzania imechaguliwa kuziwakilisha nchi za Afrika katika Baraza Tendaji la Shirika la Utalii Duniani (UNWTO), kwa kipindi cha miaka minne mfululizo kuanzia 2023 hadi 2027. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Wizara ya Maliasili na Utalii, Tanzania ilichaguliwa katika nafasi hiyo kwenye uchaguzi uliofanyika tarehe 19 Oktoba 2023, nchini Uzbekistan ambapo ilipita bila kupingwa na nchi za Afrika ambazo ni wanachama wa UNWTO.
“Tanzania imethibitishwa na Mkutano Mkuu wa 25 wa UNWTO, kuwa mjumbe wa baraza tendaji la shirika hilo kwa kuchaguliwa bila kupingwa na nchi wanachama wa Shirika la UNWTO. Uchaguzi huo umefanyika tarehe 19 Oktoba, 2023 Jijini Samarkand, Uzbekistan ambako mkutano mkuu wa 25 wa UNWTO unaendelea,” imesema taarifa hiyo.
Taarifa hiyo imesema kuwa, Afrika kupitia Tanzania itawakilishwa na Waziri wa Maliasili na Utalii, Angellah Kairuki katika mikutano muhimu ya baraza hilo inayofanyika mara mbili kwa mwaka.
“Akizungumza baada ya Tanzania kuthibitishwa katika nafasi hiyo, Kairuki ameeleza kuwa nafasi hiyo ni muhimu katika kukuza na kutangaza utalii wa Tanzania na Afrika kwa ujumla kwa kuwa Baraza hilo ni chombo muhimu kinacho simamia Mipango na Bajeti ya Shirika pamoja na utekelezaji wake,” imesema taarifa hiyo na kuongeza:
“Aidha, Waziri Kairuki ameongeza kuwa, kupitia nafasi hii, Tanzania itashiriki kupeleka agenda muhimu zenye maslahi mapana ya maendeleo ya utalii wa Bara la Afrika na duniani kwa ujumla.”
Leave a comment