SHERIA ya Bima ya Afya kwa Wote, inatarajiwa kuanza kutumika kabla ya mwisho wa mwezi Aprili 2024, baada ya vifungu muhimu kuwasilishwa katika ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG). Anaripoti Regina Mkonde…(endelea).
Hayo yamebainishwa leo tarehe 3 Aprili 2024, bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Afya, Dk. Godwin Mollel, akijibu swali la Mbunge wa viti maalum, Furaha Matondo (CCM) aliyehoji lini bima ya afya kwa watu wote itaanza kutumika.
Naibu waziri huyo wa afya, amesema baada ya sheria ya bima hiyo kupitishwa na Bunge kisha kusainiwa na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, mwezi Novemba 2023, ilichapishwa katika gazeti la Serikali tarehe 1 Disemba mwaka jana.
Amesema baada ya michakato hiyo kukamilika, Serikali ilianza maandalizi ya kuanza kutumika kwa sheria hiyo kwa waziri mwenye dhamana kuteua baadhi ya vifungu vya kuanza kutumika.
“Baadhi ya Vifungu ambavyo vinaweka mifumo imara ya kutekeleza bima ya afya kwa wote vimeshaainishwa na kuwasilishwa kwa mwanasheria mkuu wa Serikali na sheria itatangazwa kuanza kutumika kabla ya mwisho wa Aprili 2024 kwa tarehe itakayotajwa,” amesema Dk. Mollel.
Aidha, katika swali la nyongeza Matondo alihoji mkakati wa Serikali katika kuwasaidia wajane wasiokuwa na uwezo wa kulipia bima hiyo, pamoja na watoto wa mitaani.
Dk. Mollel alijibu kuwa Serikali itaangalia namna ya kuwasaidia wajane wasiokuwa na uwezo ili wapate bima hiyo, kuhusu watoto wa mitaani alisema jamii inapaswa kushirikiana kuhakikisha wanaondolewa mitaani na kurejeshwa katika familia zao.
“Moja anazungumzia kwamba nini Serikali itafanya kwa kina mama wajane ambao hawana uwezo, kwa sababu inategemea kuna mjane ambaye ana uwezo na wale wajane ambao hawana uwezo. Wabunge mnakumbuka mlisisitiza utaratibu wa kuwasaidia wasio na uwezo na utaratibu huo huo utatumika kulisaidia kundi ulilotaja,” amesema Dk. Mollel.
Leave a comment