SERIKALI imeandaa rasimu ya Mkakati wa Kitaifa wa Kutoa Elimu ya Katiba na Uraia kwa Umma, ili kuhakikisha wananchi wanafahamu haki na wajibu wao pamoja na uwezo wa kushiriki katika mijadala ya kikatiba. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Hayo yamebainishwa leo tarehe 29 Aprili 2024, bungeni jijini Dodoma na Waziri wa Katiba na Sheria, Balozi Pindi Chana, akiwasilisha mpango na makadirio ya mapato na matumizi ya wizara yake kwa mwaka wa fedha ujao wa 2024/25.
Balozi Chana amesema rasimu hiyo itajadiliwa na kufanyiwa uamuzi ndani ya Serikali kabla ya kuanza kutumika.
Katika hatua nyingine, Balozi Chana amesema katika kipindi cha Juali 2023 hadi Aprili 2024, Wizara ya Katiba na Sheria ilitoa elimu kuhusu masuala ya kikatiba na utawala wa sheria kwa umma kupitia njia mbalimbali ikiwemo vyombo vya habari na mitandao ya kijamii, ambapo wananchi 267,323 walifikiwa.
Hatua hiyo ni muendelezo wa ufufuaji mchakato wa upatikanaji katiba mpya, ambapo 2023 Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, alisema zoezi hilo litatanguliwa na utoaji elimu ya katiba kwa muda wa miaka mitatu mfululizo, ili wananchi wapate uelewa utakaowawezesha kushiriki zoezi hilo kikamilifu.
Leave a comment