MASHIRIKA Yasiyo ya Kiserikali (NGO’s), mkoani Dar es Salaam, yametakiwa kufuatia sheria za nchi katika utekelezaji wa majukumu Yao, ili kulinda maadili ya nchi. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Maagizo hayo yalitolewa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, akifungua jukwaa la NGO’s kwa 2023, likilofanyika kuanzia Jana Ijumaa Hadi Leo Jumamosi, mkoani humo.
Chalamila, aliyataka mashirika hayo kuhakikisha shughuli zao zinaleta tija katika maendeleo ya nchi na Kwa kuzingatia ustawi wa rasilimali watu.
“Kuna mashirika zaidi ya 2,700 katika mkoa wa Dar es Salaam, mengi yanapata hela lakini ukiangalia yenye tija ni machache. Inabidi fedha za wafadhili mnazopata ziendane na tija ya kazi mnazofanya. Mfano Kuna mashirika yanatetea mazingira na mabadiliko ya tabia ya nchi, lakini ukiangalia Dar es Salaam Bado chafu, hivyo yanapaswa kuendelea kutoa elimu ya utunzaji mazingira kwa Wananchi,” amesema Chalamila.
Aidha, Chalamila ameyataka mashirika hayo yatoke elimu ya kujiajiri kwa Vijana hususan wanaohitimu vyuo vikuu, ili kutatua changamoto ya ukosefu wa ajira.
Naye Msajili wa NGO’s, Vicky Mayao, amewataka viongozi wa mashirika yenye rasilimali fedha kugatua madaraka Kwa watu wengi ili kuongeza ufanisi wake.
“Unaweza kukuta shirika Lina rasilimali fedha za kutosha, lakini mtu anayefanya maamuzi ni mmoja na kama hayupo kazi haziendi. Changamoto iliyopo ni ugatuaji wa madaraka kitendo kinachowapelekea kushindwa kuzingatia sheria za nchi,” amesema Mayao.
Kwa upande wake Afisa Matekelezo Mkuu kutoka Kitengo Cha Kudhibiti Fedha Haramu nchini, Walter Mweyo, ameyataka mashirika hayo kukwepa kujiingiza katika vitendo vya utakatishaji fedha na kufadhili ugaidi, kwani ni kinyume cha sheria.
Leave a comment