WAZIRI wa Fedha, Dk. Mwigulu Nchemba amewasilisha mwongozo wa maandalizi ya mpango na bajeti ya 2024/25, bungeni jijini Dodoma, akisema Serikali imepanga kukusanya na kutumia Sh. 47.42 trilioni. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Dk. Mwigulu amewasilisha mwongozo huo leo tarehe 6 Novemba 2023, bungeni jijini Dodoma, akisema makadirio hayo yamezingatia vigezo mbalimbali ikiwemo mwenendo halisi wa ukusanyaji mapato, viashiria vya uchumi jumla na jitihada zinazochukuliwa na Serikali kuboresha mifumo ya ukusanyaji mapato.
“Katika mwaka 2024/25, Serikali inatarajia kukusanya na kutumia jumla ya Sh bilioni 47,424.9 (Sh. 47.42 trilioni). Makadirio ya mapato yamezingatia vigezo mbalimbali. Aidha, kwa upande wa matumizi, makadirio yamezingatia mahitaji halisi ya ugharamiaji wa deni la Serikali, mishahara ya watumishi pamoja na utekelezaji wa miradi ya kielelezo na kimkakati inayoendelea,” amesema Dk. Mwigulu.
Waziri huyo wa fedha amesema mapato ya ndani ikijumuishwa ya mamlaka za serikali za mitaa, yanakadiriwa kuwa Sh. 34.43 trilioni, ambapo mchango wake katika bajeti unatarajiwa kuwa asilimia 72.6.
Dk. Mwigulu ametaja vipaumbele vya bajeti hiyo, ikiwemo uendelezaji na utekelezaji miradi ya kilelezo, hususan mradi wa kufua umeme wa maji wa Julius Nyerere, kuboresha Shirika la Ndege Tanzania (ATCL), ujenzi wa reli ya kati kwa kiwango cha kimataifa (SGR), ujenzi bomba la mafuta ghafi kutoka Hoima Uganda hadi Tanzania.
Vipaumbele vingine ni, uimarishwaji wa uwezo wa uzalishaji viwandani, ukuzaji biashara na uwekezaji na kuchochea maendeleo ya watu.
Leave a comment