CHAMA cha Wananchi (CUF), kimemtaka Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, kuunda tume maalum kwa ajili ya kuchunguza mali na utajiri wa mawaziri wake, ili kuwabaini waliojilimbikizia mali kwa njia ya ufisadi baada ya kupata madaraka. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Wito huo ulitolewa jana Jumapili na Mkurugenzi wa Habari, Uenezi na Mahusiano na Umma wa CUF, Mhandisi Mohamed Ngulangwa, siku chache baada ya Mbunge wa Kisesa, Luhaga Mpina, kuibua tuhuma hizo bungeni jijini Dodoma.
“CUF kinatoa wito kwa Rais Samia kuwamulika mawaziri wake na watendaji wengine wa Serikali yake na kufuatilia mali wanazomiliki kwa kulinganisha na hali ilivyokuwa wakati anaapishwa kuwa Rais. Kuna harufu kubwa ya Ufisadi ambayo ni vema ikachunguzwa na hatua kuchukuliwa kadri itakavyoongozwa na Uchunguzi,” alisema Mhandisi Ngulangwa.
Mhandisi Ngulangwa alisema “bado watanzania hawajasahau ufisadi katika kadhia za EPA, Richmond, Tegeta Escrow na kadhia zingine zilizodhihirisha tabia chafu ya Ufisadi ya viongozi wengi watokanao na CCM, wanapoaminiwa,”
“Namna njema kwa Rais kuonesha anachukia Ufisadi na wala hahusiki nao ni kuharakisha kushughulikia hii harufu ya ufisadi kwa kuanzia na mradi huu wa SGR na mazingira yanayohusu kandarasi baina ya Serikali na Kampuni ya Yepi Markezi ya Uturuki.”
Katika hatua nyingine, kimeitaka Serikali ifanye uchunguzi wa kina juu ya tuhuma za ubadhirifu wafedha katika ujenzi wa mradi wa Reli ya Kisasa (SGR), roti ya tatu na nne, ili kubaini ukweli wake na kisha kuchukua hatua za kisheria kwa wahusika.
“CUF kinasikitishwa na taarifa zinazoashiria ubadhirifu na ufisadi katika mradi wa reli wa SGR, kuna mambo ya msingi yanayochagiza umuhimu wa kufanyika ukaguzi mahususi au kufanyika kwa uchunguzi chini ya tume huru ya uchunguzi inayostahili kuundwa kwa ajili hiyo,” alisema Mhandisi Ngulangwa.
Leave a comment