SERIKALI inakusudia kuanza kuzipa uhuru baadhi ya taasisi za umma, ili kuongeza ufanisi wa utendaji wake. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Hayo yamebainishwa leo Jumatatu, tarehe 31 Julai 2023 na Msajili wa Hazina, Nehemiah Mchechu, akizungumza katika hafla ya uwasilishaji mkakati wa miaka 10 wa utendaji wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), jijini Dar es Salaam.
Mchechu amesema, Bodi ya Wakurugenzi ya TANESCO itakuwa ya kwanza kupewa uhuru wa mamlaka, ifikapo Septemba mwaka huu, baada ya shirika hilo kuonesha mipango mizuri ya utendaji wao.
“Rais ametoa maagizo ameturudishia mamlaka ya kuzirudishia taasisi mamlaka zake. Kuanzia Septemba TANESCO itakuwa moja ya bodi itakayoshughulika kwa mamlaka yake kamili ya uendeshaji shirika. Tunategema ajira mtamalizana nazo huko, maslahi yenu mtamalizana nayo tutakalofanya tutawabana kwenye utendaji wenu ili uwe na uwajibikaji,” amesema Mchechu.
Mchechu ametaja taasisi zitakazoguswa katika mpango huo, ikiwemo vyuo vya elimu ya juu na taasisi za kibiashara.
“Hilo litafanyika pia kwa taasisi nyingine ambazo zina mikakati mizuri, zimejipanga vizuri kama TANESCO ilivyo, hususan za kibiashara na elimu ya juu. Lakini baadae tutaendelea na taasisi zote ili tuzipe uhuru ziweze kufanya mageuzi haya ambayo tunahitaji kutokea,” amesema Mchechu.
Leave a comment