RAIS mstaafu wa Nigeria, Olusegun Obasanjo ataongoza kamati ya watu 10 katika mazungumzo kati ya Rais wa Kenya, William Ruto na kiongozi wa upinzani, Raila Odinga. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa…(endelea).
Hayo yalitangazwa jana Jumamosi, tarehe 29 Julai, kupitia tamko la pamoja la muungano wa Azimio la Umoja na Kenya Kwanza.
Kwa mujibu wa tamko hilo, kila upande utatoa watu watano kuingia katika timu ya majadiliano.
“’Sisi uongozi wa muungano wa Azimio la Umoja tumeshauriana na muungano wa Kenya Kwanza chini ya uongozi wa Mheshimiwa Olusegun Obasanjo kuhusu hali ya taifa letu, tumedhamiria kutatua tofauti zetu kwa amani kwa manufaa ya watu wetu wote,’’ taarifa hiyo ilisema.
‘’Mawasiliano zaidi ya mpango huu, yatawasilishwa kwa wakati ufaao,’’ taarifa hiyo ilieleza.
Makubaliano ya viongozi hao wawili kuunda kamati, pengine huenda ni ishara kwamba wanakaribia kufikia makubaliano kutatua mgogoro wa kisiasa ambao umekumba taifa la Kenya kutokana na maandamano ya hivi karibuni ambayo yamekuwa yakiandaliwa na muungano wa upinzani kupinga kuongezeka kwa gharama ya maisha.
Jumanne iliyopita, Ruto alisema yuko tayari kukutana ana kwa ana kufanya mazungumzo na Raila na wakati wowote.
Akizungumza na wanahabari wa Kimataifa wiki iliyopita, Raila aliishutumu serikali ya Ruto kwa kukatiza juhudi za upatanishi za Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan.
Raila alifichua kuwa Rais Samia alizuru Kenya majuma kadhaa yaliyopita, lakini hakuna mawasiliano ambayo serikali ilifanya naye kuhusu jitihada za kuwaleta pamoja Ruto na Odinga.
Chanzo cha uhakika kutoka serikali ya Tanzania ambacho hakikutaka kutajwa jina lake, kiliithibitishia BBC Swahili kwamba madai ya Raila yana ukweli.
Hata hivyo, akizungumza na wanahabari msemaji wa Ikulu ya Kenya, Hussein Mohammed alipuuza madai kwamba Ruto alikataa kukutana na Samia akidai kuwa itifaki haikuzingatiwa.
Leave a comment