RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, ametuma salamu za rambirambi kufuatia kifo cha aliyekuwa Sheikh wa Msikiti wa Idrisa, Karikoo, jijini Dar es Salaam, Sheikh Maalim, Ali Basaleh, kilichotokea jana katika Hospitali ya AgaKhan, alikokuwa anapatiwa matibabu ya maradhi ya figo na saratani. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Rais Samia ametuma salamu hizo za rambirambi leo tarehe 31 Julai 2023, kupitia ukurasa wake wa Twitter.
“Nimepokea kwa masikitiko taarifa ya kifo cha Sheikh Maalim Ali Basaleh, mwanazuoni na mwalimu katika imani. Natoa pole kwa waumini wa dini ya Kiislamu, familia, ndugu, jamaa na marafiki. Mungu ailaze roho yake mahali pema peponi. Amina,” ameandika Rais Samia.
Mbali na Rais Samia, watu mbalimbali wametuma salamu za pole kufuatia msiba wa Sheikh Basaleh, akiwemo Katibu wa Shura ya Maimamu, Sheikh Ponda Issa Ponda.
Mtoto wa marehemu Sheikh Basaleh, Abdullatif Ali Basaleh, amesema mwili wa baba yake utazikwa leo Jumatatu, saa 7.00 mchana katika makaburi ya Kisutu jijini Dar es Salaam.
Marehemu Sheikh Basaleh, alikuwa mwanauzoni na sheikh maarufu nchini.
Leave a comment