RAIS Samia Suluhu Hassan amekuwa miongoni mwa Watanzania waliohesabiwa katika zoezi la Sensa ya Watu na Makazi iliyoanza saa 6:01 usiku wa leo Jumanne tarehe 23 Agosti, 2022. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Rais Samia amehesabiwa mapema leo katika ikulu ya Chamwino jijini Dodoma na karani wa sensa ambaye awali alikuwa ameambatana na Mkurugenzi Mkuu wa ofisi ya Takwimu Tanzania (NBS), Albina Chuwa na Kamishna wa Sensa ya Watu na Makazi mwaka 2022, Anne Makinda.
Aidha, baada ya kumaliza kumhesabu, kazi iliyodumu si zaidi ya dakia 25, Rais Samia amesema, “nimemaliza kuhesabiwa, ni kweli maswali ni mengi kidogo lakini yanajibika, hakuna swali gumu.. ombi langu kwa wananchi ni kuweka taarifa zetu mapema.”
“Watu wa Takwimu, makamisaa walitoa maswali mapema, wananchi watafute hayo maswali ili waanze kutafutia majibu mapema.
“Mfano atauliza kama una bima ya afya, kadi ya NIDA namba ngapi, ukikaa nazo mkononi wanakwenda haraka. Kaya zetu wastani ni watu watano, kama hamkuwa tayari inaweza kuchukua muda mrefu,” amesema.
Leave a comment