KAMISHNA wa Sensa ya Watu na Makazi mwaka 2022, Anne Makinda amesema iwapo makarani wa sensa wakifanya kazi yao kwa ufanisi na uharaka leo tarehe 23 Agosti, 2022 watafanikiwa kutekeleza zoezi hilo kwa asilimia 15.
Pia ametoa wito kwa Watanzania kuandaa taarifa zao mapema kwa mujibu wa madodoso ya sensa ambayo awali maswali yalisambazwa na ofisi ya Taifa ya Takwimu, makamisaa na makarani. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Makinda ametoa wito huo leo Ikulu Chamwino jijini Dodoma baada ya kusimamia zoezi la sensa katika makazi ya Rais Samia Suluhu Hassan.
“Tunaomba wananchi wasituchoke na sisi wenzao hatutachoka, wasianze kulalamika kuwa leo karani hajafika hapana kwa sababu hili zoezi ingewezeka kila mtu angejihesabu lakini hilo halipo.
“Kwa hiyo sio lazima ufikiwe leo kwa sababu hili ni zoezi la siku saba. Tunaomba uvumilivu kwa wananchi,” amesema.
Amesema kwa kuwa kaya zilipewa fomu zinaweza kujaza fomu hizo na kuziacha kwa mwakilishi yeyote wa kaya ili karani atakapofika iwe rahisi kwake kujaza taarifa hizo.
“Kama una kazi yako unakwenda kazini kwako, karani anaitumia ile fomu, kama kuna mahali hajaielewa atakupigia simu… hatupendi watu wakae nyumba wakisubiri karani, leo tumeiheshimu kama siku maalumu,” amesema.
Leave a comment