MKUU wa Mkoa wa Dodoma, Rossemary Senyamule ametangaza kiama kwa waendesha magari yaendayo mikoani ambao watatupa takataka pembezoni mwa barabara zote zilizopo katika mkoa huo. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma (endelea).
Mkuu huyo wa mkoa ametoa rai hiyo jana Jumatatu wakati wa zoezi la usafi lililofanyika katika kata ya Miyuji na Mipango kwa kuwashirikisha wananchi wa kata hizo, taasisi zote zilizopo katika jiji la Dodoma pamoja na wadau mbalimbali wa usafi.
Amesema kwa kuwa Dodoma ni makao makuu ya nchi ni lazima kuzingatia usafi wa hali ya juu na kutambua wazi kuwa Dodoma inapokea wageni mbalimbali hivyo ni vyema kujenga tabia ya usafi.
Kutokana na hali hiyo Senyamule amewataka waendeshaji wa magari yote abiria yaendayo mikoani yanayopita katika mkoa wa Dodoma kuhakikisha wanakusanya taka zao na kuzitupa sehemu sahihi.
Sambamba na hilo amewataka wananchi kujenda utamadumi wa kufanya usafi bila kulazimishwa au kutozwa faini jambo ambalo ameeleza kuwa ni aibu.
Wakati huo huo Mkuu wa Kitengo cha Usafi na Mazingira Jiji la Dodoma, Dikson Kimaro amesema jiji litaendelea kuhimiza suala la usafi na kuwachukulia hatua kali za kisheria wale wote watakaokaidi.
“Kila mwananchi katika eneo lake ni lazima afanye usafi na usafi iwe tabia ya mtu kuanzia nyumbani kwake na liwe somo hata kwa watoto waliopo ndani ya familia bila kusubiri kusukumwa au kuchukuliwa hatua za kisheria” amesema Kimaro.
Leave a comment