RATIBA yamazishi ya Dk. John Pombe Magufuli, aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, imeelekeza kiongozi huyo atazikwa tarehe 24 Machi 2021, Chato mkoani Geita. Anaripoti Regina Mmonde, Dar es Salaam…(endelea).
Ratiba hiyo imetolewa na Mama Samia Suluhu Hasaan, Rais wa Tanzania leo Ijumaa tarehe 19 Machi 2021, wakati akihutubia Taifa mata baada ya kuapishwa kwake kuwa Rais wa sita wa Tanzania.
Katika ratiba hiyo, Mama Samia ametangaza siku mbili za mapumziko Jumatatu ya 22 Machi, atakapoagwa kitaifa Dodoma na 25 Machi 2021, siku ambayo atazikwa.
Mama Samia ameapishwa kushika wadhifa huo, baada ya kifo cha Dk. Magufuli kilichotokea tarehe 17 Machi 2021, katika Hospitali ya Mzena, Dar es Salaam alikokuwa akipatiwa matibabu ya matatizo ya mfumo wa umeme wa moyo.
Akitangaza ratiba ya mazishi hayo, Mama Samia amesema, ratiba hiyo itaanza kesho Jumamosi tarehe 20 Machi 2021, siku ya Jumamosi ambapo mwili wa Dk. Magufuli utatolewa katika Hospitali ya Jeshi ya Lugalo na kupelekwa kwenye Kanisala St. Peter, Oysterbay kwa ibada.
Na kisha mwili huo, utapelekwa katika Uwanja wa Uhuru kwa ajili ya kuagwa na viongozi mbalimbali.
Tarehe 21 wananchi wa Dar es Salaam watapata fursa ya kumwaga Dk. Magufuli kwenye viwanja hivyo, na kisha mwili huo utapelekwa jijini Dodoma tarehe 22 Machi 2021 kwa shughuli ya kuagwa na siku hiyo itakuwa mapumziko.
Baada ya Dodoma, Mama Samia amesema siku ya Jumanne tarehe 23 Machi 2021, mwili wa Dk. Magufuli utaagwa jijini Mwanza.
Tarehe 24 Machi 2021, mwili wa Dk. Magufuli utapelekwa Chato ambapo familia na wananchi pamoja na wale wa mikoa ya jirani, watapata fursa ya kumuaga rais wao.
Tarehe 25 Machi 2021, mwili wa Dk. Magufuli utazikwa nyumbani kwao Chato ambapo Mama Samia ametangaza siku hiyo kuwa ya mapumziko.
Leave a comment