RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amewaagiza wakuu wa mikoa na wilaya nchini, wawapange wafanyabiashara ndogo ndogo ‘wamachinga’, katika maeneo rasmi. Anaripoti Noela Shila, TUDARCo … (endelea).
Rais Samia ametoa agizo hilo leo Jumatatu, tarehe 13 Septemba 2021, akiwaapisha viongozi aliowateua jana, Ikulu ya Chamwino jijini Dodoma.
Kiongozi huyo wa Tanzania, amewaagiza wakuu hao wa mikoa na wilaya, watekeleze agizo hilo bila kutumia nguvu.
“Naagiza wakuu wa mikoa kuchukua hatua za kuwapanga vyema wamachinga na ninaposema kuwapanga vyema sitaki kuona ninayoyaona kwenye Tv, ngumi, kuchafuliana vitu na kumwaga bidhaa. Mnaweza kuchukua hatua vyema bila kuudhi wamachinga na shughuli zikiendelea,” amesema Rais Samia.
Rais Samia amesema, upangaji holela wa biashara za wamachinga, unakosesha Serikali mapato, kwa kuwa unaathiri biashara za wenye maduka wanaolipa kodi.
Amewataka wamachinga wafuate sheria za nchi wakati wakifanya biashara zao, pamoja na kufuata maelekezo wanayopewa na wakuu wa mikoa na wilaya katika maeneo yao.
“Wamachinga wamekuwa wakifanya kazi maeneo tofauti, wakuu wa mikoa na wilaya wanawapanga. Kumekuwa na watu wanapumzika kiasi kwamba wameenea kila mahali mpaka kwenye maduka,” amesema Rais Samia na kuongeza:
“Wanawaziba hadi wenye maduka wamepata mtindo wa kutoa bidhaa ndani na kuwapa wamachinga, hili linatukosesha kodi sababu mmachinga halipi kodi, mfanyabiashara analipa kodi.”
Asante kwa kuliona hili mapema zaidi.
Kwa kweli Suluhisho la kitaifa ni bora sana kuliko kushughulikia mkoa mmoja tu.
Rafiki yako,
Aliko Musa.
Real estate investment consultant