RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amesema amemteua Dk. Stergomena Tax kuwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, ili kuvunja mwiko wa wizara hiyo kutoongozwa na mwanamke. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Kiongozi huyo wa kwanza mwanamke Tanzania, ametoa kauli hiyo leo Jumatatu, katika Ikulu ya Chamwino jijini Dodoma, akimuapisha Dk. Tax pamoja na mawaziri wengine watatu, aliowateua jana.
“Nimeamua kuvunja mwiko ya muda mrefu ya kwamba wizara ya ulinzi lazima akae mwanaume mwenye misuli yake, lakini kazi ya waziri kwenye wizara ile sio kubeba mizinga au bunduki, ni kusimamia sera ya wizara. Nikaamua dada yetu nimpeleke huko,” amesema Rais Samia.
Mbali na kuuvunja mwiko wa wizara hiyo kuongozwa na wanaume, Rais Samia amesema amemkabidhi wizara hiyo Dk. Tax, kutokana na uzoefu wake alioupata serikalini na akiwa Katibu Mtendaji wa Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini Afrika (SADC).
“Na si kwa sababu ya kuvunja mila, lakini sababu ya upeo wake alioupata SADC, kipindi chote tukiwa SADC amekuwa akisimamia vyema mambo ya usalama katika ukanda. Kwa uzoefu aliyoupata kwenye sekta ya ulinzi kikanda, atasimamia huko,” amesema Rais Samia.
Leave a comment