RAIS wa Madagascar, Andry Rajoelina amejiuzulu baada ya kuthibitishwa rasmi kuwa mgombea katika uchaguzi wa urais utakaofanyika tarehe 9 Novemba 2023. Anaripoti Mlelwa Kiwale, TUDARCo kwa msaada wa Mitandao ya Kimataifa…(endelea).
Kwa mujibu wa katiba ya nchi hiyo, Spika wa Seneti anatakiwa kutwaa mamlaka ya urais katika kipindi hicho cha mpito.
Hatua hiyo ya kujiuzulu kwa rais Rajoelina sio ya kushangaza huko Madagascar kwa sababu ni wajibu wa kikatiba ikiwa rais aliyeko madarakani atawania muhula wa pili ni lazima ajiuzulu kwanza.
Andry Rajoelina, mwenye umri wa miaka 49, alituma barua yake ya kujiuzulu kwa Mahakama siku ya Jumamosi baada ya kuthibitishwa na Mahakama Kuu ya Kikatiba kama mgombea wa urais.
Jambo jipya katika hali hii ni kwamba shughuli zote za kitaifa na majukumu ya rais yataendeshwa na waziri Mkuu kwa pamoja na serikali yake.
Kikatiba Spika wa Seneti ndiye anatakiwa kutwaa mamlaka ya urais wakati mkuu wa nchi anapojiuzulu.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na mahakama ya katiba ni kwamba Spika wa Seneti, Herimanana Razafimahefa, amekataa kuchukuwa madaraka kwa sababu zake binafsi.
“Mwishoni mwa wiki iliyopita, Mahakama Kuu ya Madagascar ilichapisha orodha rasmi ya wagombea urais. Kati ya wagombea 28 katika kinyang’anyiro hicho, 13 waliidhinishwa kugombea, akiwemo Andry Rajoelina na marais wawili wa zamani, Marc Ravalomanana na Hery Rajaonarimampianina.
Upinzani umelalamikia mchakato wa maandalizi ya uchaguzi huo akiwamo Masy Goulamaly, mbunge na mgombea wa zamani wa urais ambaye amesema amejiondoa kwenye kinyang’anyiro cha uchaguzi huo.
“Kuna hitilafu nyingi katika uchaguzi huu, ugombea wa rais wa sasa unathibitisha hili kwa kushindwa kuheshimu sheria, nadhani ndiyo maana kuna uwezekano wa kutokea mgogoro, hivyo napendelea kujitoa kwenye kinyanganyiro tuone nini kitafuata.”, alisema Goulamaly.
Leave a comment