Saturday , 27 April 2024
Home Kitengo Habari Kimataifa Putin, Xi Jinping kujadili mpango kumaliza vita nchini Ukraine
Kimataifa

Putin, Xi Jinping kujadili mpango kumaliza vita nchini Ukraine

Spread the love

 

Vladimir Putin amesema atajadili mpango wenye vipengele 12 wa Xi Jinping wa “kusuluhisha mgogoro mkubwa nchini Ukraine”, wakati wa ziara inayotarajiwa mjini Moscow ya rais wa China. Imeripoti Mitandao ya Kimataifa … (endelea)

“Siku zote tuko wazi kwa mchakato wa mazungumzo,” Putin alisema, huku viongozi hao wakiitana “rafiki mpendwa”.

China ilitoa mpango wa kumaliza vita mwezi uliopita – ikiwa ni pamoja na “kukomesha uhasama” na kuanza tena mazungumzo ya amani.

Lakini siku ya Ijumaa Marekani ilionya mpango huo wa amani unaweza kuwa “mbinu ya kukwama”.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Antony Blinken alisema: “Ulimwengu haupaswi kudanganywa na hatua yoyote ya kimbinu ya Urusi, inayoungwa mkono na China au nchi nyingine yoyote, kusimamisha vita kwa masharti yake yenyewe.”

Aliongeza: “Kutoa mwito wa kusitishwa kwa mapigano ambayo haijumuishi kuondolewa kwa vikosi vya Urusi kutoka Uraine itakuwa inaunga mkono kuidhinishwa kwa ushindi wa Urusi.”

Mpango wa China haukusema haswa kwamba Urusi lazima ijiondoe kutoka Ukraine – ambayo Ukraine imesisitiza kama sharti la mazungumzo yoyote.

Badala yake, ilizungumzia “kuheshimu mamlaka ya nchi zote”, na kuongeza kuwa “wahusika wote lazima wawe na busara na wajizuie” na “kupunguza hali hiyo pole pole”.

Mpango huo pia umelaani matumizi ya “vikwazo vya upande mmoja” – vinavyoonekana kama ukosoaji uliofichika kwa washirika wa Ukraine katika nchi za Magharibi.

Siku ya Jumatatu, bendi ya kijeshi ilimkaribisha Xi kwa furaha mjini Moscow. Putin aliipongeza China kwa “kuzingatia kanuni za haki” na kushinikiza “usalama usiogawanyika kwa kila nchi”.

Kwa upande wake, Xi alimwambia Bw Putin: “Chini ya uongozi wako dhabiti, Urusi imepiga hatua kubwa katika maendeleo yake yenye ustawi. Nina imani kwamba watu wa Urusi wataendelea kukupa uungaji mkono thabiti.”

Kabla ya kuwasili kwa Xi, Putin aliandika katika gazeti la People’s Daily la China kwamba mataifa hayo mawili hayatadhoofishwa na sera ya “uchokozi” ya Marekani.

Hadharani, viongozi wa Ukraine wamekuwa wakisisitiza msingi wa pamoja walio nao na China – kuheshimu uhuru wa nchi huru.

Lakini kwa faragha, wamekuwa wakishawishi mkutano – au simu – kati ya Rais Volodymyr Zelensky na Xi.

Hofu katika Kyiv ni kwamba uungaji mkono wa China kwa Urusi – ambao kwa sasa umeegemezwa katika teknolojia na biashara – unaweza kuwa wa kijeshi, uwezekano wa kujumuisha makombora.

“Ikiwa China itachukua hatua ya kusambaza silaha kwa Urusi, itakuwa ikishiriki katika mzozo kwa upande wa mvamizi,” alisema Oleksiy Danilov, katibu wa Baraza la Usalama na Ulinzi la Kitaifa la Ukraine.

Ilikuwa ni kwa manufaa ya Beijing kuleta utulivu katika uhusiano na Urusi, ambayo inashiriki mpaka wa kilomita 4,300 (maili 2,700), alisema Yu Jie, mtafiti kuhusu China katika Chatham House.

Urusi ni chanzo cha mafuta kwa uchumi mkubwa wa Beijing, na inaonekana kama mshirika katika kusimama dhidi ya Amerika.

Yu aliongeza kuwa Xi alikuwa ametoka tu kupata ushindi wa kidiplomasia katika upatanishi kati ya Iran na Saudi Arabia, ambazo sasa zimerejelea uhusiano wa kidiplomasia.

Hii inaweza kuwa nafasi kwake kutafuta fursa ya kupatanisha Urusi na Ukraine.

Siku ya Jumatatu jioni, Xi alipatiwa mlo ikiwa ni pamoja na samaki wa nelma kutoka Mto Pechora kaskazini mwa Urusi, supu ya vyakula vya baharini ya Kirusi ya kitamaduni na chapati na kware – pamoja na divai ya Kirusi.

Msemaji wa rais Dmitry Peskov alionyesha kutakuwa na “maelezo ya kina” ya hatua za Moscow nchini Ukraine wakati wa chakula cha jioni. Wajumbe wa Urusi na China watafanya mazungumzo Jumanne – siku kuu ya ziara hiyo.

Mkutano huo unakuja siku chache baada ya Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC) kutoa hati ya kukamatwa kwa rais wa Urusi kutokana na tuhuma za uhalifu wa kivita.

Hii inamaanisha kuwa Putin anaweza kukamatwa kitaalam katika nchi 123 – ingawa Uchina au Urusi haziko kwenye orodha hiyo.

Kufanya safari ya kwenda Moscow mara tu baada ya tangazo la ICC inaashiria kuwa China “haina jukumu la kuiwajibisha Urusi” kwa ukatili nchini Ukraine, Bw Blinken alisema.

Viongozi wa nchi za Magharibi wamekuwa wakijaribu tangu Februari mwaka jana kuitenga Urusi, kufuatia uvamizi wake nchini Ukraine.

Lakini wameshindwa kuanzisha makubaliano ya kimataifa, huku China, India na mataifa kadhaa ya Afrika yakisita kumshutumu Putin.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za SiasaKimataifaTangulizi

Tanzania, Somalia kuibua maeneo mapya ya ushirikiano

Spread the love  RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, amesema Tanzania na Somalia...

KimataifaTangulizi

Mkuu wa majeshi Kenya afariki, Ruto atangaza maombolezo

Spread the loveRais wa Kenya, William Ruto ametangaza maombezo ya siku tatu...

Kimataifa

Majaji kuamua hatima ya Zuma leo

Spread the loveMajaji nchini Afrika Kusini leo Jumanne wataamua ikiwa rais wa...

Habari za SiasaKimataifa

Spika Afrika Kusini ajiuzulu kwa tuhuma za rushwa

Spread the loveSpika wa Bunge la Afrika Kusini, Nosiviwe Mapisa-Nqakula ametangaza kujiuzulu...

error: Content is protected !!