Friday , 3 May 2024
Home Kitengo Biashara Prof. Kitila asisitiza uwekezaji hatifungani ya kijani
Biashara

Prof. Kitila asisitiza uwekezaji hatifungani ya kijani

Spread the love

WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo ametoa rai kwa wananchi, kampuni za sekta binafsi na umma, taasisi za serikali kutoka ndani na nje ya nchi kuwekeza katika hatifungani ya kijani au “Green Bond” ya Benki ya CRDB. Anaripoti Selemani Msuya…(endelea).

Profesa Kitila ametoa raia hiyo leo Alhamisi wakati wa hafla ya uzinduzi wa Hatifungani ya Kijani uliofanyika katika Hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam na kuhudhuriwa na watu wa kada mbalimbali wa ndani na nje ya nchi.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Prof. Kitila Mkumbo (katikati) akikabidhi Kitabu kwa Afisa Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA), Nicodemus Mkama, ikiwa ni ishara ya uzinduzi wa kuanza kutoa hatifungani ya kijani “green bond” yenye jumla ya thamani ya dola za kimarekani milioni 300 sawa na Shilingi bilioni 780 kutoka Benki ya CRDB ikiwa ni ya kwanza kutolewa Tanzania na ya kwanza kwa ukubwa Kusini mwa Jangwa la Sahara, katika hafla iliyofanyika leo kwenye hoteli ya Serena, jijini Dar es salaam. Wengine pichani ni Mwenyekiti wa Bodi ya Benki ya CRDB, Dkt. Ally Laay (watatu kulia), Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya Benki ya CRDB, Prof. Neema Mori (kushoto), Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela (watatu kushoto), Mwakilishi kutoka Benki Kuu ya Tanzania, Robert Mshiu (wapili kushoto) pamoja na Naibu Afisa Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA), Mary Mniwasa.

Amesema uamuzi wa Benki ya CRDB kuja na hatifungani hiyo ya kijani na kutoa fursa kwa wananchi na taasisi mbalimbali kununua hisa na fedha zitakazopatikana kuelekezwa kwenye miradi ya mazingira ni wa kuigwa na taasisi nyingine kwani unaenda kusaidia serikali kutekeleza miradi mingi.

Kitila amesema serikali ina mipango mingi ya kuhakikisha miradi ya kuzuia uharibifu wa mazingira unaosababishwa mabadiliko ya tabianchi kutokea, hivyo ujio wa Kijani Bond ni wazi kuwa lengo hilo litaweza kutumia.

“Kijani Bond inaenda kugusa miradi ya mazingira, afya, elimu, maji na mingine mingi, hivyo nichukue nafasi hizi kuziomba taasisi zingine za kifedha na zisizo za kifedha kuunga mkono juhudi hizo za CRDB,” amesema.

Waziri huyo amesema ujio wa hatifungani hiyo ya kijani sio tu kwamba unanufaisha miradi tajwa, ila hata wawekezaji wenyewe ambapo benki imeweka bayana kuwa itatoa riba ya zaidi ya asilimia 10.2 kwa kila mwekezaji ambaye atawekeza kuanzia shilingi 500,000 ndani ya siku 37 kuanzia leo.

Amesema Serikali itatoa ushirikiano na taasisi yoyote ambayo itajikita kwenye uwekezaji ambao unagusa jamii, kwa kuwa lengo lake ni kuongeza ajira na kipato kwa wananchi na nchi kwa ujumla.

“CRDB inafanya kile ambacho sisi tunakipigania kuongeza ajira, kipato na kuitangaza nchi, leo hii wapo hadi Burundi, DR Congo na hili la hatifungani ya kijani linaenda kugusa dunia kwa ujumla,” amesema.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu Mkuu wa CRDB, Abdulmajid Nsekela amesema fedha ambazo zitapatikana kupitia hatifungani ya kijani zitatumika kufanikisha miradi yenye mrengo wa kuhifadhi mazingira hali ambayo itaifanya Tanzania iendane na mikakati ya dunia ya kupambana na mabadiliko ya tabianchi.

“Agosti 18, 2023 ilikuwa siku moja ya siku za furaha sana kwa Benki ya CRDB baada ya Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA) kutupa idhini ya kuuza hatifungani ya kwanza ya kijani Tanzania na kubwa zaidi kwa nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara.

Lakini naweza kusema leo tupo katika kilele cha furaha kwa kuwa sasa tunakwenda kuaza kuunza hatifungani za kijani nawaomba Watanzania na wasio watanzania kuchangamkia fursa hii,” amesema.

Nsekela amesema kamilika kwa mchakato huu ulioanza mapema mwaka jana ni mafanikio makubwa kwao kwani wataalamu wao wa ndani na nje ya Benki yetu walilazimika kufanya kazi usiku na mchana kukamilisha taratibu za kikanuni na kisheria.

Mkurugenzi Mkuu huyo amesema jitihada hizi zisingefaa kitu kama si ushirikiano ambao tulipata kutoka CMSA ambao hawakuchoka kuwapa miongozo mpaka leo hii wanaanza kuiuza hatifungani yao.

“Kufanikiwa kuanza kuuza hatifungani hii kubwa zaidi kwa nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara, ni heshima kwa nchi yetu kwa kuwa Benki ya CRDB ni benki ya kizalendo inayomilikwa na Mtanzania mmoja mmoja, Serikali pamoja na taasisi zake. Na hili linaendelea kudhihirisha kuwa taasisi zetu zina uwezo wa kufanya mambo makubwa katika ulingo wa kimataifa,”amesisitiza.

Nsekela amesema msukumo wa benki hiyo kuuza hatifungani ya kijani umejikita katika ushiriki wao wa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi ambayo yameleta athari duniani kote.

“Kwa kutambua umuhimu na mahitaji yaliyopo, Benki ya CRDB iliona ni muhimu kutafuta vyanzo vipya vya fedha ili kuwezesha miradi hii ndipo lilipopatikana wazo la hatifungani ya kijani.

Hatifungani hii ambayo CMSA imetupa idhini ya kuiuza ina thamani ya dola milioni 300 za Marekani sawa na takribani shilingi bilioni 780 za Tanzania ambayo kama nilivyosema awali hii ni kubwa zaidi kuwahi kutolewa katika nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara,” amesema.

Amesema hatifungani hii itakayoorodheshwa katika Soko la Hisa Dar es Salaam (DSE) na Soko la Hisa London yaani London Stock Exchange (LSE), wanatarajia kuiuza kwa awamu na katika awamu hii ya kwanza mauzo yanaanza leo, Agosti 31, 2023 na yatadumu kwa siku 37 mpaka Septemba 6 na matarajio ni kukusanya Shilingi Bilioni 55.

Nsekela amesema kufanikiwa kuuzwa kwa hatifungani hiyo kutakwenda kuiongezea uwezo mkubwa Benki  kuwezesha wawekezaji ambao miradi yao katika namna moja au nyingine inasaidia katika utunzaji wa mazingira.

Amesema hili ni eneo ambalo wameshuhudia mataifa mengi duniani yanawekeza huko ambapo hapa Afrika tayari nchi kama Afrika Kusini, Ghana, Nigeria na Kenya tayari wamepiga hatua kubwa.

Akizungumzia umuhimu wa Watanzania kuwekeza katika hatifungani ya kijani Nsekela amesema ambapo kiwango cha chini ni shilingi 500,000.

“Sambamba na hilo, hatifungani hii ya kijani ni uwekezaji ambao una uhakika wa kukulipa au kwa lugha ya kigeni wanasema “risk free investment”. Kupitia uwekezaji wa hatifungani ya kijani ya Benki ya CRDB, muwekezaji atakua na uhakika wa kupata riba ya asilimia 10.25 ambayo ni biashara chache sana ambazo unaweza kuzifanya na ukawa na uhakika wa kupata kiasi hiki tena bila kujali mazingira ya biashara yatakuaje,” amesema.

Mwenyekiti wa Bodi ya CRDB, Alhaj Ali Lawi amesema benki hiyo itaendelea kuboresha huduma zake, ili kuhakikisha kila anayepata huduma ananufaika.

Ofisa Mtendaji Mkuu wa CMSA, Nicodemus Mkama amesema kinachofanywa na CRDB ni cha kuigwa na kila taasisi ya kifedha kwani kina faida kwa jamii kwa ujumla.

Mkama amesema ili Tanzania iweze kuendelea ni jukumu la kila taasisi kuja na bunifu mbalimbali za kuwezesha jamii nzima inashiriki kwenye uchumi.

“CMSA tupo tayari kushirikiana na taasisi yoyote ambayo itakuja na wazo ambalo linataka kuwakwamua wananchi na nchi kwa ujumla, CRDB imeonesha njia tuiunge mkono benki yetu kwa kununua hisa za hatifungani ya kijani,”amesema.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

BiasharaHabari Mchanganyiko

NMB yang’ara maonesho OSHA

Spread the loveBenki ya NMB imebeba tuzo ya kampuni bora kwenye sekta...

BiasharaHabari Mchanganyiko

NBC yashiriki maadhimisho Mei Mosi Arusha

Spread the loveBenki ya Taifa ya Biashara (NBC) imeungana na maelfu ya...

Biashara

Promosheni ya bil 1 kutoka Meridianbet kasino, cheza na ushinde zawadi kubwa

Spread the love  INGIA katika ulimwengu wa zawadi za kushangaza: Jishindie sehemu...

BiasharaHabari Mchanganyiko

Equity Bank yaendelea kusotea mabilioni ya fedha mahakama rufani

Spread the loveBENKI za Equity ya Tanzania na Kenya, zimeendelea kupambana mahakamani...

error: Content is protected !!