Mwenyekiti wa Ngome ya Vijana ya Chama cha ACT-Wazalendo Abdul Nondo na wenzake wanne huenda wakafikishwa mahakamani tarehe 25 Machi kwa tuhuma za kufanya vurugu kwenye uchaguzi wa marudio wa Kata ya Kasingirima baada kumkamata kijana mfuasi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) waliyemuona na kura ‘feki’. Anaripoti Faki Sosi… (endelea).
Mbali na Nondo, viongozi na wanachama wengine wa Kigoma Mjini ambao wanatarajia kuburuzwa mahakamani ni pamoja na Mgombea udiwani kata ya Kasingirima, Alumbula Khalidi; Alhaji Mzee Selemani Simba, Ntakije Ntanena na Khamis Mzungu.
Makada hao wa ACT wazalendo walikamatwa na polisi siku ya uchaguzi katika kata ya Kasingirima- Kigoma Mjini tarehe 20 Machi 2024 baada ya kumzuia kijana wa anayedaiwa kuwa mfuasi wa CCM akiwa na kura bandia.
Akizungumza MwanaHALISI Online leo Jumamosi, Mwenyekiti wa ACT-Wazalendo, Abdul Nondo amesema wamefunguliwa kesi na muda wowote kuanzia sasa wanaweza kupelekwa Mahakamani wakituhumiwa kufanya fujo katika kituo cha kupigia kura cha Mtaa wa Livingston -Kasingirima.
Amesema pia wanatuhumiwa kumshambulia kijana wa CCM, tuhuma ambazo amedai kuwa sio za kweli.
“Tumetakiwa wote kurejea Central Police Kigoma siku ya Jumatatu tarehe 25 Machi 2024. Nimewasilisha malalamiko yangu kwa OCD Kigoma Mjini na kufungua jalada la kesi kwa OCCID dhidi ya Polisi kituo kikuu aliyetumia”Unreasonable Force”dhidi yangu kwa kunipiga kinyume na PGO No. 15 na 16 tarehe 20/03/2024.
“Ni katika uchaguzi wa Kasingirima baada ya kutaka kijana aliyekuwa na kura bandia akamatwe. Nitafuata taratibu zote hadi hatua stahiki zichukuliwe dhidi ya Askari huyu.
“Sioni mwanga mbele kwenye uchaguzi wa serikali ya mtaa 2024 na uchaguzi Mkuu 2025, sababu maneno ya kuleta mabadiliko yamekuwa mengi kuliko vitendo,” amesema.
Amesema chaguzi hizo za marudio hazina tofauti na chaguzi za 2019 na 2020.
“Wasimamizi wa vituo wote ni viongozi na wanachama wa CCM. Napata wakati mgumu kushawishika kwamba uchaguzi wa 2024 na 2025 kama utakuwa tofauti,” amesema na kuongeza;
“Wananchi, vyama vya upinzani, Asasi za kiraia na watu wote bado tuna kazi kubwa ya kushinikiza mabadiliko ya vitendo hasa katika chaguzi na kuepuka kuamini maneno ya watawala na CCM.”
Leave a comment