CHAMA Cha Mapinduzi (CCM), kimefanikiwa kupata ushindi katika uchaguzi wa marudio uliofanyika tarehe 20 Machi mwaka huu, kwenye kata zote 23 za Tanzania Bara. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Kupitia taarifa iliyotolewa jana Ijumaa na Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM, Idara ya Oganaizeshi, Issa Haji Ussi, chama hicho kimewashukuru wawapiga kura wa kata hizo kwa kukipa ushindi kwa asilimia 89.
“CCM inawaahidi watanzania kuendelea kuwatumikia kwa uaminifu na uadilifu pamoja na kusimamia serikali katika kila hatua ya utekelezaji wa ilani ya uchaguzi ya mwaka 2020-2025. Aidha, CCM inawasihi watanzania wote kuendelea kuiamini na kuipa fursa CCM na serikali yake iweze kuendelea kuwatumikia watanzania kwa ufanisi mkubwa,” imesema taarifa hiyo.
Taarifa ya Ussi imesema mafanikio ya ushindi huo ni kutokana na umoja na mshikamano uliopo ndani ya CCM, uteuzi wa wagombea bora, kampeni za kistaarabu na kisayansi zilizowafikia wapiga kura.
“Uaminifu na uadilifu katika kuwatumikia wananchi hususan katika kukidhi mahitaji na matarajio yao katika kuwaletea maendeleo, kazi ambayo inafanywa kwa weledi na ustadi mkubwa na serikali ya awamu ya sita chini ya mwenyekiti Rais Samia Suluhu Hassan, kupitia utekelezaji wa ilani ya uchaguzi,” imesema taarifa hiyo.
Miongoni mwa kata zilizofanya uchaguzi mdogo ni, Kimbiji (Dar es Salaam), Kasingirima (Kigoma), Chipuputa (Mtwara), Buzilasoga (Mwanza), Mkuzi (Tanga), Mbingamhalule (Ruvuma) na Kibata (Lindi).
Leave a comment