Sunday , 5 May 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Nape: Hakuna aliyeripoti kuibiwa bando, muda wa maongezi
Habari za Siasa

Nape: Hakuna aliyeripoti kuibiwa bando, muda wa maongezi

Nape Nnauye, Waziri wa Habari, Mawasiliano na Tekinolojia
Spread the love

 

WAZIRI wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye, amesema licha ya kutoa ofa kwa mwananchi yeyote aliyeibiwa vifurushi vya intaneti au muda wa maongezi na mitandao ya simu, hakuna yeyote aliyewasilisha malalamiko kwake.

Pia amesema kwa mujibu wa tafiti zilizofanywa na taasisi za kimataifa, Tanzania inashika nafasi ya sita kwa Bara la Afrika kwa kuwa na gharama za chini za bando “vifurushi” huku ikishika nafasi ya 32 Duniani kwa gharama ya chini ya data. Anaripoti Erick Mbawala, TUDARCo … (endelea).

Waziri Nape ametoa ufafanuzi huo wakati aliposhiriki kipindi cha Power Breakfast on Saturday cha Clouds TV na redio, leo tarehe 20 Agosti, 2022 jijini Dar es Salaam.

Amesema bei ya data kwa wastani wa 1GB ni Dola 1.71 sawa na shilingi 3,990.

“Tanzania kuwa miongoni mwa Mataifa yenye gharama za chini za mawasiliano haimaanishi kuwa itapunguza malalamiko kwa kuwa uchumi wetu haufanani na wananchi wengi wana kipato cha chini”, amesema Waziri huyo na kuongeza;

“Nilitoa ofa kama kuna mtu amehisi kuibiwa aje tumsaidie apate ushahidi wa hiyo taarifa, bahati mbaya, wengi wakija wakifanyiwa tathmini wanaondoka hawataki kuweka wazi na wengine ni viongozi,” amesema.

Amesema kuwa Serikali kupitia Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imeendelea kufanya tathmini ya gharama za uwekezaji, utunzaji na usafirishaji wa data kila baada ya miaka minne na tathmini nyingine inafanyika mwaka huu ili kupata uhalisia wa gharama za bando kama zitapanda au kushuka.

“Wananchi wanatakiwa kufahamu kuwa Serikali yao ni sikivu na inafanyia kazi malalamiko na maoni ya wananchi, lakini pia nitoe rai kwa wananchi kuwa makini na matumizi ya simu janja hasa kwenye kujiunga na huduma mbalimbali pamoja na program tumizi “applications” ili kupunguza matumizi ya bando”, Amesisitiza Waziri Nape

Aidha, Waziri Nape amesema kuwa Serikali imeruhusu ushindani kwa kuweka mazingira wezeshi ya kuwa na kampuni nyingi zinazotoa huduma za mawasiliano ambapo huduma ya vifurushi ni huduma ya ziada inayotolewa na makampuni hayo na kuleta unafuu wa gharama za mawasiliano.

Ameongeza kuwa kwa ulimwengu wa sasa wa kidijiti huduma nyingi zinapatikana kwa njia ya mtandao, hivyo kuifanya huduma ya intaneti kuwa huduma muhimu na ya msingi katika kuendesha shughuli za uzalishaji na upatikanaji wa huduma za kijamii.

Katika hatua nyingine Waziri Nape ameielekeza TCRA, Baraza la Watumiaji wa Huduma za Mawasiliano (TCRA- CCC) na Makampuni ya simu kuendelea kutoa elimu kwa wananchi na kujibu au kutoa ufafanuzi wa maswali na malalamiko ya wananchi.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za SiasaTangulizi

Mbatia ambwaga Selasini, mahakama yaamuru alipwe fidia

Spread the loveMAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam, imemuamuru...

Habari za SiasaTangulizi

Mkulo afariki dunia, kuzikwa kesho Kilosa

Spread the loveALIYEKUWA Waziri wa Fedha na Mbunge wa Kilosa (CCM), Mustafa...

Habari za SiasaTangulizi

Sabaya afutiwa kesi, ruksa kugombea uongozi

Spread the loveMwendesha Mashtaka Mkuu wa Serikali DPP leo Ijumaa amefuta rufaa...

Habari za Siasa

Serikali yasaka bilioni 3 kujenga daraja Mto Mpiji

Spread the loveSerikali imesema inaendelea na juhudi za kutafuta fedha kiasi cha...

error: Content is protected !!