OFISI ya Msajili wa Vyama vya siasa nchini, inaendelea na zoezi la uhakiki wa masharti ya usajili wa vyama hivyo, ambapo hadi sasa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) na Chama cha ACT-Wazalendo, vimefikiwa na zoezi hilo. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Chadema kimefanyiwa uhakiki leo Alhamisi, tarehe 3 Agosti 2023,wakati ACT-Wazalendo, kikihakikiwa jana Jumatano.
MwanaHALISI Online, imemtafuta Naibu Msajili wa Vyama vya Siasa, Sisty Nyahoza, ili kupata taarifa zaidi kuhusu zoezi hilo, ambaye amesema atatoa taarifa za awali kuhusu matokeo ya uhakiki huo kesho Ijumaa.
“Zoezi linaendelea na tayari Chadema na ACT-Wazalendo vimeshahakikiwa, kuhusu matokeo ya uhakiki nakushauri ungepiga kesho jioni maana tutakuwa tumeshamaliza wiki. Kwa sasa tunafanya uhakiki wa vyama vingine hivyo kesho itakuwa rahisi kufanya tathimini ya zoezi kisha kutoa taarifa ya awali,” amesema Nyahoza.
Mtandao ulimtafuta Katibu Mkuu wa ACT-Wazalendo, Ado Shaibu, kwa ajili ya kupata maoni yake kuhusu zoezi hilo, ambaye alijibu “wanaopaswa kusema ni ofisi ya msajili, nashauri ongeeni na msajili, sisi tukizungumza sasa haitakuwa vyema kuongea kabla wao hawajatoa matokeo ya uhakiki.”
Kwa mujibu wa ratiba ya zoezi hilo iliyotolewa na Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa, zoezi hilo linatarajiwa kufungwa tarehe 15 Agosti mwaka huu, ambapo Chama Cha Mapinduzi (CCM), kitahakikiwa jijini Dodoma.
Ratiba hiyo inaonyesha orodha ya vyama vya siasa 19, vitakavyohakikiwa katika nyakati tofauti kuanzia tarehe 2 hadi 15 Agosti mwaka huu.
Leave a comment