TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) mkoa wa Mwanza imebaini uwepo wa kasoro katika mradi wa elimu wa ujenzi wa vyumba vitatu vya madarasa katika shule ya msingi Sumbuka wilayani Misungwi. Anaripoti Moses Mseti, Mwanza … (endelea).
Mradi huo wenye thamani ya Sh. 60,000,000 unadaiwa kujengwa chini ya kiwango na tayari Takukuru imeanza kuchukua hatua za kufungua jalada la uchunguzi.
Mradi huo wa elimu ni kati ya miradi 37 ya maendeleo yenye thamani ya zaidi ya Sh. 112 bilioni iliyofayiwa ukaguzi na Takukuru mkoa wa Mwanza.
Kaimu Mkuu wa Takukuru mkoa wa Mwanza, Leonidas Rugemalila, alisema katika kipindi cha Aprili hadi Juni 2019 imefanya ukaguzi katika miradi hiyo na ikiwemo wa mradi mkubwa wa ujenzi wa meli mpya katika ziwa Victoria wenye thamani ya dola za kimarekani 39 milioni.
“Lengo kuu la ufuatiliaji huu ni kuhakikisha miradi inatekelezwa kwa kiwango kinachotakiwa na thamani ya fedha inaonekana kwa kuzuia mianya ya rushwa na upotevu wa rasilimali katika utekelezaji wake.
“Katika kutekeleza majukumu yake Takukuru mkoa wa Mwanza kwa kipindi cha Aprili hadi Juni 2019, imeweza kuokoa kiasi cha Sh. 8,332,680 milioni na kudhibiti upotevu wa fedha kiasi cha Sh. 28,249,249.12 milioni,” alisema Rugemalila.
Katika hatua nyingine, Rugemalila alisema katika kipindi hicho cha Aprili hadi Juni kumekuwepo na malalamiko ya vitendo vya rushwa, ambapo serikali za mitaa inaongoza kwa kuwa na malalamiko 33 kati ya 175 waliopokea.
Rugemalila alisema idara nyingine inayofuatia kwa malalamiko ni idara ya elimu yenye malalamiko 20, ardhi 17, Polisi 15, Mahakama 14 na Taasisi za fedha 9.
Alisema Takukuru imejipanga kuongeza kasi ya ufuatiliaji wa karibu na ukaguzi wa kina katika miradi ya maendeleo ili kuhakikisha inatekelezwa katika ubora uliokusudiwa kudhibiti vitendo vya rushwa.
Pia amegusia uchaguzi mkuu unaotarajia kufanyika Oktoba mwaka huu kwa kuwataka wananchi kuchagua viongozi wenye uwezo wa kuwaletea maendeleo sio wenye uwezo wa kutoa rushwa ili wachaguliwe.
Leave a comment